BONDIA mtanzania Hassani Mwakinyo anatarajia kushuka ulingoni 13 Novemba, 2020 kutetea mianda wake wa chama cha WBF dhidi ya bondia Raia wa Argentina, Jose Carlos katika pambani la uzito wa Super Welter. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Pambano hilo limepewa jina la Dar Fight Night ambalo limeandaliwa na Jackson Group Sports litafanyika kwenye ukumbi wa Next Door Arena uliopo Masaki jijini Dar es Salaam.
Katika mkutano na waandishi wa Habari Mwakinyo amesema kuwa anashauku kubwa na pambano hilo kutokana na maandalizi aliyoyafanya kiasi cha kutaka pambano hilo lifike kwa haraka kwani tayari ameshamsoma vya kutosha mpinzani wake.
“Nimepata nafasi ya kumuona mpinzani wangu naamini ni bondia mzuri na mzoefu na mara nyingi huwa wanabadilika kutokana na mechi, hata akifanya maandalizi kutoka mbinguni ila kwa kuwa ameshafika nitampiga,” alisema Mwakinyo.
Mbali na kutetea mkanda wake Mwakinyo pia atawania ubingwa wa mabara wa uzito huo huo wa chama cha IBA.
Kwa upande wa mpinzani wake, Jose Carlos alimjibu Mwakinyo kwa kusema kuwa mpaka sasa maandalizi yake yanakwenda vizuri na anamini kuwa atauchukua mkanda huo kwa kuwa hata yeye pia anapiga ngumi nzito.
“Nimefurahi kupata nafasi hii kwa kuwa nimefanya mazoezi na nimejiandaa vizuri na nitahakikisha nitauchukua mkanda huo kwa kuwa hata mimi pia napiga ngumi nzito,” alisema bondia huyo.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa kampuni ya Jackosn Group Sports, Kelvin Twissa ambao ndio waandaaji wa pambano hilo, amesema kuwa kabla ya Mwakinyo na Jose Carlos kupanda ulingoni kutakuwa na mapambano ya utangulizi kwa mabondia kutoka nchi sita tofauti.
Leave a comment