MAALIM Seif Sharif Hamad, mgombea urais wa Zanizbar kupitia ACT-Wazalendo amesema, ana matumaini Tundu Lissu ataibuka mshindi wa urais wa Tanzania kupitia Chadema katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Vivyo hivyo yeye mwenyewe (Maalim Seif) amesema, atamshinda kwa mbali, mgombea urais visiwani humo kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Dk. Hussein Ali Mwinyi.
Maalim Seif amesema hayo leo Jumamosi tarehe 3 Oktoba 2020 wakati akizindua timu ya ushindi wa Ngoma ya Wanawake wa ACT-Wazalendo visiwani humo huku akiwapa jukumu la kusaka kura kwa njia ya kisayansi.
Amesema, Chama Cha Mapinduzi (CCM) si kwamba hakikubaliki Zanzibar bali hata Tanzania Bara jambo ambalo linamfanya mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia CCM, Rais John Pombe Magufuli atashindwa na Lissu.
“Haiwezekani Hussein Mwinyi ashinde urais Zanzibar, hata CCM wenyewe hawamtaki sasa atashindaje,” amehoji Maalim Seif aliyewahi kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanizbar.
“Hata kampeni zenyewe zimemshinda, anakutana na makundi makundi na hata wajane nasikia amewaita na kukutana naye. Sasa atanishindaje mimi? Hussein Mwinyi hawezi kunishinda,” amesema Maalim Seif
Katika kusisitiza hilo, Maalim Seif amesema “kwa hali ilivyo CCM imechoka, hawawezi kushinda, Zanzibar Rais atakuwa Maalim Seif na Rais wa Jamhuri ya Muungano awamu hii atakuwa Tundu Lissu, woga umezidi wanamfungia, wamfungulie kwani moto aliouwasha Lissu sasa hivi hawamwezi tena kuuzima.”
“Nataka baada ya miaka mitano yangu ya urais niwaache Wazanzibar wakiwa na maisha mazuri, yenye raha na furaha,” amesema
Ametumia mkutano huo, kuwaomba wanawake hao kuhakikisha wanapiga kampeni usiku na mchana ili kujihakikishia ushindi kabla ya uchaguzi ambao kwa Zanzibar utafanyika kwa siku mbili tarehe 27 na 28 Oktoba 2020.
Leave a comment