FLUGENCE Massawe, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu nchini Tanzania (LHRC), ameshauri mamlaka husika (Wizara ya Mambo ya Ndani) kutatua utata ulioibuka dhidi ya Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
“LHRC tunaamini kwamba, mamlaka husika zitalishughulikia suala hili kwa haraka, ili kuiwezesha taasisi ya THRDC kuendelea na kazi zake,” inaeleza taarifa iliyotolewa na Massawe kwa vyombo vya habari leo tarehe 19 Agosti 2020.
Aidha, LHRC imeeleza kuwa, imeshtushwa na taarifa za THRDC kusitisha shughuli zake huku ikitoa pole kwa uongozi wa mtandao huo kufuatia changamoto inazopitia wakati huu.
Soma zaidi:-
- Ni hofu, woga THRDC?
-
THRDC yasitisha shughuli zake
“LHRC tumeshtushwa sana na taarifa zilizotolewa na THRDC kuhusu kusitisha shughuli zake kwa muda kufuatia kufungwa kwa akaunti za benki za taasisi hiyo.”
“Tunatoa pole kwa Bodi ya Wakuruenzi mratibu na wanachama kwa usumbufu wanaoupitia,” imeeleza taarifa ya LHRC.
THRDC uliitangazia umma wa Tanzania tarehe 17 Agosti 2020 kwamba unasitisha shughuli zake, baada ya kukumbwa na changamoto za kifedha za uendeshaji, kufuatia akaunti yake katika Benki ya CRDB kufungwa na Jeshi la Polisi.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Vicky Ntetema, Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya THRDC , Jeshi la Polisi limefunga akaunti hiyo, ili kufanyia kazi masuala yaliyoko mbele yake.
Hata hivyo, taarifa hiyo inaeleza kwamba, Onesmo Ole Ngurumwa, Mratibu wa THRDC siku ya Jumatatu alihojiwa na Jeshi la Polisi kuhusu tuhuma zinazo kabili mtandao huo, za kutowasilisha mikataba yake na wafadhili katika Ofisi ya Hazina na Ofisi ya Msajili wa Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s).
Leave a comment