SHIRIKA la Reli Tanzania (TRC) limesema, ndani ya siku 14 zijazo, litarejesha safari za treni za mizigo na abiria kati ya Dar es Salaam na Moshi mkoani Kilimanjaro baada ya kuzisitisha kwa muda kutokana na mafuriko ya mvua. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa iliyotolewa jana Alhamisi tarehe 4 Juni 2020 na Jamila Mbarouk, Mkuu wa Kitengo cha habari na Uhusiano wa TRC ilisema, mafuriko hayo ya mvua yalisababisha mto Pangani kujaa.
Alisema, mvua hizo zilinyesha katika maeneo ya mkoa wa Kilimanjaro na nchi jirani ya Kenya hivi karibuni Mei 2020.
“Mafuriko hayo yamesababisha uharibifu wa miundombinu ya reli kati ya Stesheni ya Buiko na Hedaru ambapo kipande cha reli chenye urefu wa Kilomita 1.6 kilifunikwa na maji kwa zaidi ya siku 21,” alisema Jamila
Alisema, kutokana na hali hiyo, TRC lilisitisha kwa muda safari za treni za abiria na mizigo kati ya mikoa ya Dar es Salaam, Tanga na Kilimanjaro kuanzia tarehe 10 Mei 2020 ambapo baadaye Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Masanja Kadogosa alifanya ziara katika eneo hilo akiambatana na timu ya wataalamu wa shirika ili kuona maendeleo ya utengenezaji wa njia hiyo.
Jamila alisema, tathimini iliyofanywa na wataalamu wa TRC kukamilisha utengenezaji na kurejesha njia hiyo katika hali ya usalama na hatimaye safari za treni kwenda Moshi kuanza tena.
Alisema, shirika hilo linaendelea na kazi ya kuinua tuta la reli kati ya Stesheni ya Buiko na Hedaru ambapo matengenezo yataratajia kukamilika ndani ya siku 14 tangu kuanza kwa kazi hiyo tarehe 1 Juni 2020.
Leave a comment