WANASIASA kadhaa wanahojiwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), kwa tuhuma za kujihusisha na vitendo vya rushwa, katika mchakato wa maandalizi ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Regina Mkonde. Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Ijumaa, tarehe 15 Mei 2020, na Brigedia Jenerali, John Mbungo, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU wakati akizungumza na wanahabari kuhusu majukumu ya taasisi hiyo na shughuli ambazo wanazifanya.
Brigedia Mbungo amesema wanasiasa hao wanahojiwa baada ya kugundulika wanajihusisha na vitendo vya rushwa, ili kuwarubuni watu wawaunge mkono katika mchakato wa uteuzi, kwa ajili ya kugombea nafasi mbalimbali, ndani ya vyama vya siasa.
Mkurugenzi huyo wa TAKUKURU amedai kuwa, wahusika wanahojiwa kwa makosa ya kufanya kampeni kabla ya muda.
“Tunao watu kadha wa kadha tunaowahoji, tumebaini wanafanya vitendo si vya kiungwana, wanapita mitaani wakijaribu kuwaandaa watu kwa ajili ya kuwapigia chapuo la kuwateua. Tunaendelea kuwahoji, na wale wanaobainika kufanya vitendo vya rushwa, tunawachukulia hatua,” amesema Mbungo alipokuwa akijibu swali la mmoja wa waandishi waliohoji mikakati ya Takukuru kuendelea uchaguzi mkuu
tayari, baadhi ya vyama vya siasa vimeshaanza mchakato wa kupata wagombea wake katika uchaguzi huo, ambapo wanachama wameshaanza kutangaza nia ya kutaka kugombea katika nafasi mbalimbali ikiwamo za udiwani, ubunge na uwakilishi wa upande wa Zanzibar.
Miongoni mwa vyama ambavyo vimefungua dirisha la utiaji nia ya kugombea, ni Chama cha Wananchi (CUF), Chama cha ACT-Wazalendo, Chama cha Ukombozi wa Umma (Chaumma), Chama cha NCCR Mageuzi. Huku Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kikifunga mchakato huo tangu tarehe 30 Machi 2020.
Chama tawala cha Mapinduzi (CCM), bado hakijafungua mchakato wa utiaji nia kwa ajili ya kugombea nafasi mbalimbali, ambapo kinatarajia kufungua milango baada ya Bunge kuvunjwa.
Kanali Ngemela Lubinga, Katibu wa Siasa na Uhusiano wa Kimataifa wa CCM, akizungumza na Mwanahalisi Online kwa simu, amesema chama hicho kitafungua rasmi mchakato wa utiaji nia, baada ya bunge kuvunjwa.
“CCM watu wataanza kutangaza nia baada ya Rais John Magufuli kulivunja Bunge tarehe 29 Mei 2020. Kwa sasa ni marufuku kwa sababu bado kuna wabunge halali,” amesema Kanali Lubinga.
Leave a comment