CHAMA cha Wananchi (CUF) kimelalamikia zoezi la uandikishaji wa Daftari la Wapiga kura, kikieleza kwamba lina kasoro. Anaripoti Hamis Mguta… (endelea).
Malalamiko hayo yametolewa leo tarehe 30 Septemba 2019 jijini Dar es Salaam na Abdul Kambaya, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Umma CUF, wakati akizungumza na wanahabari.
Kambaya amesema chama hicho kimebaini kasoro kwenye vigezo vya kujiandikisha katika daftari hilo, vilivyowekwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC),.
Kambaya ameeleza kuwa, kigezo cha mtu kujaza namba yake ya simu katika daftari hilo, ni kikwazo kwa baadhi ya wananchi wasiokuwa na simu hasa, wale wa maeneo ya vijijini.
“Tume isiweke vigezo vya kuandika namba ya simu kwenye kujiandikisha katika daftari la kudumu la mpiga kura, huko vijijini kuna watu wengine hawana simu,” amesema Kambaya.
Pia, Kambaya amesema kigezo cha mtu kuwa na kitambulisho cha taifa au cha mpiga kura, kinaweza sababisha vitendo vya udanganyifu, kama hakitasimamiwa ipasavyo.
“Vigezo vya mtu kuwa na kitambulisho ama leseni, tunadhani hapa ni pa kusimamia. Mpiga kura wa mtaa anatambulika na watu wa mtaa, na sio kitambulisho. Kwa sababu ni rahisi mtu kudanganya, ni kikwazo kitakacholeta mgongano baina ya wananchi katika chaguzi hizi,” amesema Kambaya.
Kambaya ametaja kasoro nyingine kuwa ni, kigezo cha mgombea kuwa na chanzo cha mapato, na kueleza kwamba, hakuna mfumo unaothibitisha mtu kama ana kipato halali.
“Kigezo kingine ni mgombea lazima awe na kipato halali, kijijini kumkuta mtu ana kipato halali ni ngumu. Kwa sababu, kwa tafsiri kipato halali ni kinachomwezesha mtu kulipa kodi,” amesema Kambaya na kuongeza.
“Hakuna mfumo mzuri wa kodi huko vijijini. Hiki ni kipengele kinacholeta tabu, wagombea wetu kuthibitisha kuwa wana kipato halali ni ngumu sana. Mazingira yanayotengenzwa na tume ni ya kibaguzi, kwa sababu kipengele hiki hakipo kwa ajili ya mpiga kura.”
Wakati huo huo, Kambaya amekanusha kauli ya Kangi Lugola, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, ya kwamba hajapokea malalamiko kutoka kwa vyama vya siasa kuzuiwa kufanya mikutano na Jeshi la Polisi.
Kambaya amesema chama cha CUF kilinyimwa kufanya mikutano wakati chama cha CCM kikiruhusiwa kufanya mikutano ya siasa.
“Sisi tuliwahi kuomba kibali cha mikutano na tukanyimwa, wakati haya yakiendelea CCM wanaendelea na Dar es Salaam ya kijani. Mizengo Pinda alikuwa Mtwara, kwenye Mtwara ya kijani, lakini sio diwani wala mbunge,” amesema Kambaya.
Kambaya ameipongeza hatua ya Rais John Magufuli kuwasamehe wahujumu uchumi, na kumuomba aruhusu mikutano ya hadhara.
“Rais kama juzi aliweza kutoa tamko la kusamehe wahujumu uchumi na walipe pesa, hii ni jambo la busara na si la sheria. Kutokana na hilo, lilikuwa mahakamani maana yake ametumia busara kutatua tatizo. Na kwenye mikutano ya adhara napo anatakiwa afanye busara,” amesema Kambaya.
Leave a comment