WANACHAMA wa Chama cha United Peoples Democratic Party (UPDP), wameitaka Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa nchini, kutovibomoa vyama vya siasa vya upinzani. Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 13 Januari 2020, kutokana na maelezo kwamba chama hicho kina mgogoro wa kiuongozi, baada ya Katibu wa Chama hicho kutangaza kumvua Fahmi Dovutwa uenyekiti wa chama hicho.
Asha Chuma, Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya UPDP, ameitaka ofisi hiyo kuwa msimamizi na mlezi wa vyama vya siasa, badala kutengeneza migogoro.
“Mfululizo wa matukio haya na mengine yanaonesha kuwa, mgogoro huu ndani ya chama umechagizwa na umetenegezwa na msajili wa vyama vya siasa.
“… kama ambavyo amekuwa akifanya katika vyama vingine kuanzia mwaka 2015 hadi mwaka huu. Kwa mtazamo wetu, hivi sasa ameacha kutekeleza majukumu yake yaliyopo kisheria ambayo ni kulea vyama na kuanza kuvibomoa,” amesema Chuma.
Chuma amesema, uamuzi wa ofisi hiyo kutambua kikao batili kilichodai kumvua uenyekito Dovutwa, umeonesha wazi kwamba iko nyuma ya mgogoro huo.
Nassoro Lugome, Mwenyekiti wa UPDP, Mkoa wa Dar es Salaam amemtaka Katibu Mkuu wa UPDP, kushirikiana na mwemyekiti wake, Dovutwa kuitisha mkutano mkuu wa chama kwa ajili ya kujadili mustakabali wa chama hicho.
Mbwana Kibanda, Mweka Hazina wa UPDP amesema, wataendelea kumtambua Dovutwa kama mwenyekiti wa chana hicho, hadi pale mkutano mkuu utakapoamua vinginevyo.
Kibanda amesema, Katiba ya UPDP inamtambua Dovutwa kama mwenyekiti halali wa chama hicho.
Leave a comment