TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU) imemfukuza kazi Cosmas Batanyita, aliyekuwa Mchunguzi Mwandamizi wa taasisi hiyo, kwa kosa la kuomba na kupokea rushwa. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Hayo amesema Kamishna wa Polisi Diwani Athumani, Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU wakati akizungumza na wanahabari leo tarehe 9 Agosti 2019 jijini Dar es Salaam.
Kamishna Athumani amesema Batanyita alikuwa mchunguzi mwandamizi katika makao makuu ya ofisi za TAKUKURU jijini Dar es Salaam.
“Tunapenda kuutarifu umma kuwa tumemkamata afisa wa TAKUKURU aitwaye Cosmas Revelian Batanyita, alikuwa mchunguzi mwandamizi makao makuu ya ofisi ya Dar es Salaam kwa kosa la kuomba na kupokea rushwa, na amefukuzwa kazi,” amesema Kamishna Athumani.
Wakati huo huo, Kamishna Athumani amewaonya matapeli wanaojifanya maafisa wa TAKUKURU kujipatia fedha kutoka kwa wananchi, akisema kwamba taasisi hiyo imejipanga kukabiliana nao.
Kamishna Athumani amesema hivi sasa kuna wimbi la matapeli wanaojifanya ni maafisa wa TAKUKURU na vyombo vingine vya ulinzi na usalama, wanaotumia mbinu mbalimbali kuomba hongo kutoka kwa wananchi.
“Matapeli hawa wamekuwa wakitumia mbinu mbalimbali ikwia pamoja na kupigia simu wananchi wakitaka wapewe hongo ili wasichukuliwe hatua wakidai kuwa wanakabiliwa na makosa ya rushwa. Wale wote wanaotaka kuchafua taswira chanya ya TAKUKURU kuacha mara moja tabia hiyo yenye lengo la kuondoa imani ya wananchi kwa serikali yao,” amesema Kamishna Athumani.
Aidha, Kamishna Athumani amewataka wananchi kuwa makini na watu wanaojitambulisha kwao kwamba ni maafisa wa TAKUKURU.
“Ni rai yangu kwenu, mwananchia usikubali kudanganywa na yeyote yule bila kumdadisi japo kwa kumtaka ajitambulishe kwako ikiwezekana akupatie kitambulisho ama akueleze kosa lako, hii ni haki.
TAKUKURU haifanyi kazi zake vichochoroni, afisa wa TAKUKURU hufanya kazi zake za kiuchunguzi huwa na kitambulisho pamoja nayaraka anazopewa na ofisi kufanya upelelezi nje ya ofisi,” amesisitiza Kamishna Athumani.
Leave a comment