WAKILI Simba Richmomd Akaro Neo, amechukua fomu ya kugombea Urais wa Tanzania, kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Wakili Simba amekabidhiwa fomu hiyo leo Ijumaa tarehe 10 Julai 2020 katika Makao Makuu ya Chadema, Kinondoni jijini Dar es Salaam na Reginald Munisi, Mkurugenzi wa Uchaguzi Chadema.
Mtia nia huyo anakuwa wa tano ndani ya Chadema kugombea Urais wa Tanzania, tangu zoezi hilo lianze tarehe 4 Julai 2020. Zoezi hilo litafungwa tarehe 19 Julai mwaka huu.
Waliomtangulia ni Dk. Mayrose Majinge, Tundu Lissu, Makamu Mwenyekiti Chadema, Lazaro Nyalandu, Mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Kati, Wakili Gaspar Mwalyela, Isaya Mwitta, aliyekuwa Meya wa Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam.
Baada ya kukabidhiwa fomu hiyo, Wakili Simba ametaja mambo atakayoyafanya endapo atapitishwa na Chadema kugombea nafasi hiyo, kisha kuchaguliwa kuwa Rais wa Tanzania.
Wakili Simba ameahidi kuboresha vyombo vinavyosimamia haki, ikiwa pamoja na kuifanya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), inakuwa huru katika kupambana na wala rushwa.
“Ahadi yangu ni kukuza demokrasia, kuipatia Takukuru uhuru katika kufanya kazi zake na kurudisha hadhi ya Tanzania Kimataifa,” amesema Wakili Simba.
Wakati huo huo, Wakili Simba amesema akifanikiwa kupitishwa na Chadema kugombea Urais wa Tanzania, kisha kuchaguliwa na Watanzania, atahakikisha maendeleo na demokrasia vinaenda pamoja.
“Tusiwe tunaongelea maendeleo bila demokrasia, ukiwa na moja tu ni ulemavu, ni muhimu kwamba demokrasia na maendeleo yanakwemda sambamba,” amesema.
Aidha, Wakili Simba ameishauri Chadema kutowachagua wanasiasa walioshika nafasi za uongozi serikalini kwa muda mrefu, kwa maelezo kwamba wamechokwa na wananchi.
Leave a comment