MBUNGE wa Ilala (CCM), Mussa Azan Zungu, ametumia Kanuni za Bunge toleo la 2020, kuomba wabunge wamchague katika kiti cha U-Naibu Spika. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Tukio hilo limetokea leo Ijumaa, tarehe 11 Februari 2022, bungeni jijini Dodoma, wakati Zungu anajibu maswali ya wabunge, baada ya kuomba kura.
Mbunge huyo wa Ilala aliulizwa maswali matatu, ambapo yote aliyajibu huku akitaja kanuni hizo.
Mbunge wa kwanza kumuuliza Zungu, alikuwa Cecil Mwambe (Ndanda), aliyemhoji “ulikuwa mbunge wa muda mrefu ndani ya Bunge na sasa unatuomba kura uwe Naibu Spika wa Bunge hili, tunataka kusikia kutoka kwako nini hasa unataka kufanya ili kuliboresha bunge letu.”
Zungu alijibu swali hilo akisema, majukumu ya Naibu Spika yameanishwa katika Kanuni za Bunge, Toleo la 2020 na kuwa anafanya kazi kwa maelekezo ya Spika wa mhimili huo,Dk. Tulia Ackson.
“Kazi za Naibu Spika zimeainishwa kwenye toleo la 2020 za Kanuni za Bunge, ambazo wote tumezipitisha mwezi wa sita. Majukumu yangu yameainishwa na mimi nafanya kazi chini ya Spika, kwa maelekezo yoyote akiyatoa Spika,” amesema Zungu.
Naye Mbunge wa Kalenga, Jackson Kiswaga, alimuuliza akiwa Naibu Spika wa Bunge, atawasaidiaje wabunge kutimiza ahadi zao kwa wananchi.
“Sisi wabunge kama wawakilishi wa wananchi, wananchi wetu wamekuwa na matarajio makubwa sana na kile ambacho tunaweza ku-deliver (kutoa) ni kidogo kulingana na kile wanachotarajia. Wewe kama Naibu Spika utatusaidiaje wabunge ili tuweze kufanya kazi zetu vizuri majimboni kusukuma kazi ambazo tumeaminiwa na wananchi?” amesema Kiswaga.
Zungu alijibu swali hilo akisema “Toleo la 2020 limeanisha majukumu yangu, maelekezo yoyote yatakayotolewa na Spika katika kuboresha mahusiano ya wabunge ndani ya Bunge na nje ya Bunge, ndiyo nitakayofanya.”
Aidha, Zungu amewataka wabunge wajikite katika kusimamia miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali.
“ Niwaombe, Serikali yetu kwa kipindi hiki chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, wana pesa nyingi za miradi. Wabunge lazima tujue namna ya kusimamia miradi, hilo nitachukua maelekezo kutoka kwa Spika ni namna gani tushirikiane tuhakikishe pesa za wananchi zinatumika ipasavyo,”amesema Zungu.
Awali Zungu aliwaomba wabunge wamchague katika kiti cha Naibu Spika wa Bunge, kwa kuwa kazi za mhimili huo alizozifanya wanazifahamu.
Zungu ni mgombea pekee wa nafasi hiyo, baada ya kupitishwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM), huku vyama vingine, vyama vingine vya upinzani vikishindwa kuweka mgombea.
Nafasi ya Naibu Spika wa Bunge, iliachwa wazi baada ya aliyekuwa anaishikilia, Dk. Tulia kujiuzulu na kugombea U-Spika, baada ya Job Ndugai kujiuzulu.
Leave a comment