SIKU chache baada ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kutoa wito kwa watumiaji wa huduma za Mawasiliano ya simu, kuhakiki laini zao za simu Mamlaka hiyo imeeleza kuwa kumekuwa na mwitikio chanya wa uhakiki wa laini za simu kutoka kwa watumiaji wa huduma za Mawasiliano huku ikiwaasa wasiokamilisha zoezi la uhakiki kufanya hivyo kabla ya mwezi January kutamatika. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mapema mwezi Desemba 2022, mamlaka hiyo kupitia taarifa ya Mkurugenzi Mkuu Dk. Jabiri Bakari ilieleza kuwa lengo la zoezi la uhakiki wa laini za simu zinazotumika ni kuwalinda watumiaji wa huduma za Mawasiliano dhidi ya matukio ya utapeli na wizi mtandaoni miongoni mwa sababu nyingine.
“Kila mmoja wetu akitekeleza kwa ukamilifu zoezi hili tutafanikiwa kuweka anga la Mtandao wa Mawasiliano, hasa Mawasiliano ya simu nchini, kuwa salama zaidi kwa kila mmoja wetu,” alisisitiza.
Meneja wa Kitengo cha Usimamizi wa Mawasiliano ya simu na Intaneti wa Mamlaka hiyo Mhandisi Sadath Kalolo akizungumzia Maendeleo ya zoezi hilo litakalofikia ukomo mwishoni mwa Januari 2023 amesema kuwa kati ya laini za simu 60,076,000 zinazotumika zilizosalia kuhakikiwa ni laini 2,061,000 sawa na asilimia 4.3.
Awali katika Taarifa ya Mkurugenzi Mkuu TCRA ilielekeza kuwa kwa kubofya namba *106# katika simu, yako utaweza kuhakiki usajili wa namba yako ya simu, pamoja na kutazama idadi ya namba za simu zilizosajiliwa kwa namba yako ya kitambulisho cha Taifa kinachotolewa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).
“Baada ya kupiga namba *106# utapewa chaguzi kadhaa namba 1 hadi 5, ukichagua namba 3 utaweza kutazama idadi ya namba za simu zilizosajiliwa kwa namba yako ya Uraia iliyotolewa na NIDA. Mtumiaji wa huduma za mawasiliano ya simu za mkononi akibaini namba za ziada, zaidi ya zilizosajiliwa kwa namba yake ya NIDA, atatakiwa kuchukua hatua,” ilielekeza taarifa hiyo.
Mamlaka hiyo imebainisha kuwa baadhi ya watumiaji huduma za mtandao wa simu wamekuwa wakikwepa kusajili laini za simu kwa sababu mbalimbali, ikiwemo kukwepa kubainishwa kwa matendo ya jinai wanayotenda kwenye mtandao hivyo hutumia mbinu ya kununua laini za simu zilizosajiliwa tayari kwa utambulisho wa watumiaji wengine wa huduma za Mawasiliano.
Mapema mwezi Novemba mwaka jana TCRA ilitangaza kuzifungia jumla ya namba tambulishi 52,087, zikiwemo zile zinazohusishwa na wizi, utapeli na ulaghai kupitia mitandao wa simu; ambapo imesisitiza kampeni ya uhakiki wa laini za simu inayofanyika kipindi hiki inafanywa kwa ushirikiano na watoa huduma wote wa mitandao ya simu na kwamba baada ya Januari 31 mwaka huu wasiotekeleza zoezi la uhakiki laini zao zitazuiliwa kutoa na kupokea huduma.
Leave a comment