WIZARA ya Afya imetaja mafanikio 10 iliyoyapata ndani ya miaka mitatu ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, aliyeingia madarakani Machi 2021, kufuatia kifo cha mtangulizi wake Hayati Dk. John Magufuli. Anatipoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Akitangaza mafanikio hayo, leo Jumatatu, jijini Dar es Salaam, Waziri wa Afya,Ummy Mwalimu, amesema yamekuja baada ya Serikali ya Rais Samia kuipa wizara hiyo kiasi cha Sh. 6.72 trilioni, ndani ya miaka mitatu.
Ummy ametaja mafanikio hayo ikiwemo uboreshaji miundombinu ya kutoa huduma za afya, ununuzi wa vifaa tiba vya kisasa, ongezeko la vitanda vya wagonjwa wa kawaida na mahututi, uimarishaji upatikanaji wa dawa muhimu, uboreshaji huduma ya afya ya uzazi, mama na mtoto.
Mengine ni kupungua vya vifo vya wanawake wajawazito kwa asilimia 80. Huduma za ubingwa na ubingwa ubobezi kuimarika, ongezeko la rasilimali watu katika sekta ya afya, uboreshaji huduma za dharura na ajali, pamoja na mapambano dhidi ya magonjwa wa UKIMWI, Kifua kikuu na malaria
“Tukifanya mapitio ya miaka mitatu ya Rais Samia, naweza kusema sekta ya afya tunakwenda vizuri, tunakwenda mbele, namba zinatubeba, kwa hiyo nitumie fursa hii kumshukuru Rais wetu kwanza kwa maono yake, pili kwa maelekezo yake ya mara kwa mara katika kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa Tanzania, lakini tatu tunamshukuru na kumpongeza Rais wetu kwa kutupatia raslimali fedha nyingi,” amesema Ummy.
Leave a comment