SERIKALI ya Zanzibar, imekamilisha mchakato wa uchimbaji wa mafuta na gesi asilia baharini ambapo imeanza kutangaza utoaji wa leseni za uchimbaji na vitalu kwa wawekezaji. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo tarehe 18 Machi 2024 na Waziri wa Uchumi wa Buluu na Uvuvi Zanzibar, Shaaban Ali Othman, akitangaza uzinduzi wa duru ya kwanza ya zoezi la utoaji vitalu, utakaofanyika tarehe 20 Machi mwaka huu, visiwani humo.
Waziri huyo amesema uzinduzi huo unajiri baada ya zoezi la uchakataji data za ugawaji vitalu vipya vya maeneo ya bahari yaliyopo Mashariki mwa Zanzibar, kukamilika, pamoja na mabadiliko ya Sheria Namba 6 ya 2016 na mapitio ya modeli ya mkataba wa ugawaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia ya 2017.
“Nikiwa waziri mwenye dhamana ya mafuta na gesi asilia, nafurahi kuwajulisha maandalizi yanayohitajika ili Zanzibar kuanza kutoa vitalu vya wawekezaji kwa ajili ya utafutaji na uchimbaji mafuta na gesi asilia sasa imekamilika, ina maana kwamba sasa Zanzibar iko tayari kwa duru ya kwanza ya utoaji vitalu katika maeneo ya baharini kwa wawekezaji duniani kote,” amesema Othman.
“Hatua hii ya duru ya utangazaji vitalu itafungua fursa kwa wawekezaji zitakazopelekea kuimarika kwa uchumi wa Zanzibar pia kuiweka Zanzibar katika ramani ya dunia katika sekta ya mafuta na gesi asilia.”
Leave a comment