SAFARI ya kuwania ubunge, uwakilishi (Zanzibar) na udiwani ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kwenye uchaguzi mkuu wa tarehe 28 Oktoba 2020, itahitimishwa tarehe 22 Agosti 2020. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Siku hiyo majina yaliyopenya ili kuingia kwenye karatasi ya kupigia kura yatawekwa hadharani, lakini pia yalioanguka nayo yatajulikana. Kura za maoni ndani ya chama hicho zilifanyika kwa siku mbili – tarehe 20 – 21 Julai 2020.
Tayari CCM imeeleza mara kadhaa kwamba, kura za maoni zilizopigwa na wanachama wa chama hicho katika hatua ya awali, ni kutoa picha halisi ya eneo husika na si hitimisho.
Hata hivyo, takribani wabunge 36 wa CCM walianza vibaya safari yao ya kutetea nafasi zao baada ya kushindwa kwenye kura hizo. Nao wanatega sikio ili kujua kifuatacho.
Miongoni mwa wabunge walioshindwa katika hatua hiyo ya awali na sasa wanasubiri huruma ya vikao vya juu ni pamoja na aliyekuwa mbunge wa Babati Vijijini, mkoani Manyara, Jitu Soni; aliyekuwa mbunge wa Mufindi Kusini, mkoani Iringa, Medard Kigola na mwenzake wa Kilolo, Venance Mwamoto.
Wengine walioangukia pua ni aliyekuwa mbunge wa Kyera, mkoani Mbeya, Dk. Harrison Mwakyembe; aliyekuwa mbunge wa Babati Mjini, mkoani Manyara, Pauline Gekul; aliyekuwa mbunge wa Serengeti, mkoani Mara, Mwalimu Chacha Marwa Ryoba; aliyekuwa mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, Omary Mgumba na Balozi Diodorus Kamala, aliyekuwa mbunge wa Nkenge.

Dk. Mwakyembe na Mgumba ni mawaziri katika serikali ya Rais John Pombe Magufuli. Wakati Dk. Mwakyembe akiwa waziri kamili wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mgumba ni naibu waziri wa kilimo.
Katika orodha hiyo wamo aliyekuwa mbunge wa Ileje (Songwe), Janeth Mbene; aliyekuwa mbunge wa Mwanga (Kilimanjaro), Prof. Jumanne Maghembe; aliyekuwa mbunge wa Ndanda (Masasi, Mtwara), Cecil Mwambe; aliyekuwa mbunge wa Misungwi (Mwanza), Charles Kitwanga na aliyekuwa mbunge wa Kasulu Mjini, mkoani Kigoma, Daniel Nswanzugwako.
Wengine walioshindwa kura za maoni, ni Selemani Sadiq Murad (Mvomero), Peter Lijualikali, aliyekuwa mbunge wa Kilombero, Goodluck Mlinga, aliyekuwa mbunge wa Ulanga, wote wakitokea mkoa wa Morogoro.
Dk. Shukuru Kawambwa, aliyekuwa mbunge wa Bagamoyo, mkoani Pwani, Albert Obama, aliyekuwa mbunge wa Buhigwe, mkoani Kigoma na Godfrey Mgimwa, aliyekuwa mbunge wa Kalenga, mkoani Iringa.
Pia wamo waliokuwa wabunge kutoka vyama vya upinzani na kuhamia CCM kwa madai ya kuunga juhudi za Rais John Magufuli kwenye utawala wake. Miongoni mwao ni aliyekuwa mbunge wa Temeke, Abdallah Mtolea; aliyekuwa mbunge wa Liawale, mkoani Lindi, Zuberi Kuchauka na aliyekuwa mbunge wa Kinondoni, Maulid Mtulia.
CCM imetoa ratiba yake kuelekea uteuzi wa mwisho wa wateule wake ambapo Kikao cha Sekretarieti ya Halmashauri Kuu kitakutana leo na kesho, pia kikao cha Kamati ya Usalama na Maadili ya Taifa kitafanyika.
Kuelekea kitanzi za wagombea, kikao kitachofuata ni cha Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya Taifa kitakachofanyika tarehe 20-21 Agosti 2020.

Kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa ya CCM ambacho ndio cha hitimishi ya safari ya jasho kwa wagombea wa ngazi hizo, kitafanyika Jumamosi ya tarehe 22 Agosti 2020.
Wakati CCM ikiendelea kupitia nyaraka za lundo la wagobea wake, baadhi ya vyama vya upinzani vimeanza kuchukua fomu za kugombea nafasi hizo tatu kwenye maeneo yao.
Tayari dirisha la uchukuaji fomu kwa nafasi za ubunge, udiwani na uwakilishi limefunguliwa. Miongoni mwa vyama ambavyo vimeanza kuchukua fomu ni pamoja na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema).
Leave a comment