WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais-Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Ummy Mwalimu amewataka wakurugenzi (DED) wapya 69 walioteuliwa kufika makao makuu ya ofisi hizo, Dodoma kesho Alhamisi, tarehe 5 Agosti 2021. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Kati ya wakurugenzi hao watendaji 184 wa Halmashauri za Jiji, Manispaa,Miji na Wilaya waliteuliwa tarehe 1 Agosti 2021 na Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, 69 ni wapya.
Miongoni mwa walioteuliwa ni wanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambao baadhi walijitosa kwenye uchaguzi ndani ya chama hicho kuwania ubunge wa majimbo ama viti maalum kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika mwaka 2020.
Wakurugenzi hao wanatakiwa kufika ofisini hapo saa 3:00 asubuhi, wakiwa na vyeti vya kuzaliwa, kitambulisho Nida, wasifu binafsi (CV), vyeti vya kitaaluma pamoja na picha mbili (passport size).
“Wakurugenzi ambao wahehamishwa vituo na wale walioendelea kuwepo kwenye vituo vyao vya awali waendelee na utaratibu wa kwenda kuripoti kwenye vituo vyao vya kazi kwa ajili ya makabidhiano kuanzia tarehe 3 Agosti 2021,” imeeleza taarifa ya Tamisemi iliyotolewa na Nteghenjwa Hoseah, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa ofisi hiyo
Taarifa hiyo imesema, wakurugenzi ambao uteuzi wao umesitishwa “wakaripoti kwa makatibu tawala mikoa yao mara moja.”
Mmoja wa waliowahi kuwa watumishi wa umma aliyeomba hifadhi ya jina lake amezungumzia taarifa hiyo ya Waziri Ummy akisema “inawezekanaje mtu umwambie aende na CV au kitambulisho cha Nida, kwani wakati anateuliwa haya hayakuzingatiwa?”
“Nafasi ya mkurugenzi ni nyeti sana, huyu ndiye anakwenda kusimamia mapato, katibu wa baraza la madiwani, sasa unapomteua mtu bila kumjua sijui utumishi wa umma tunauweka katika mazingira gani,” amesema
Leave a comment