BAADHI ya Wazee wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), mkoani Njombe, wamempa zawadi Mwenyekiti wao Taifa, Freeman Mbowe, kwa kutambua mchango wake katika ujenzi wa chama hicho. Anaripoti Mwandishi Wetu, Njombe … (endelea).
Tukio hilo limetokea leo Jumatatu, tarehe 27 Februari 2023, katika mkutano wa hadhara wa Chadema, uliofanyika mkoani Njombe.
Akielezea sababu za wazee hao kumtunuku Mbowe, Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake la Chadema (Bawacha), wilaya ya Wanging’ombe, Amina Limari, amesema wamemfunga shuka jeupe na kilemba cheupe, pamoja na kumkabidhi mkuki mdogo, kama heshima ya kumkaribisha kutokana na ushujaa wake.
“Wazee zaidi ya 300 wako hapa kwa ajili ya kumpokea Mbowe kama mwenyekiti wetu taifa na kumuunga mkono kwa maumivu makali aliyoyapata. Sisi tupo pamoja naye. Kumfunga shuka kama heshima ya kumkaribisha shujaa wetu na kumfunga kilemba cha ushujaa. Pia tuna zawadi ndogo ya mkuki kama alama ya ushujaa wake,” amesema Amina na kuongeza:
“Pia, kuna chakula cha supu ya kuku aliyenona kwa ajili ya kurutubisha afya yake.”
Baada ya Mbowe kukabidhiwa zawadi hiyo, Mkurugenzi wa Itifaki, Mawasiliano na Mambo ya Nje Chadema, John Mrema, alimtaka DJ kuweka wimbo wa Mbowe sio gaidi, ulioimbwa na msanii Mwingira.
Miongoni mwa misukosuko aliyopitia Mbowe, ni tukio la kukaa mahabusu ya Gereza la Ukonga, jijini Dar Es Salaam, takribani miezi minane, akikabiliwa na mashtaka ya ugaidi, pamoja na walinzi wake watatu.
Mbowe aliyekamatwa na Jeshi la Polisi Julai 2021 jijini Mwanza, aliachwa huru na Mahakama Kuu, Kitengo cha Rushwa na Uhujumu Uchumi, jijini Dar es Salaam, Machi 2022 baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP), kuwasilisha hati mahakamani hapo ya kutokuwa na nia ya kuendelea na mashtaka hayo.
Leave a comment