SERIKALI imesema inaendelea kuwalipa pensheni ya ulemavu wazee 272, waliopigana vita ya Kagera 1979. Anaripoti Jemimah Samwel, Dar es Salaam…(endelea).
Hayo yamesemwa leo tarehe 9 Novemba 2023, bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk. Stergomena Tax, akimjibu Mbunge Viti Maalum (CCM), Fakharia Shomar, aliyehoji Serikali inatoa kauli gani kuhusu kuwasaidia walioapata ulemavu wakati wa kupigana katika vita hiyo.
Dk. Tax amesema, mbali ya wazee hao kulipwa pensheni, wanaendelea kupatiwa matibabu kwenye hospitali za jeshi, pamoja na kupata stahiki nyingine kwa mujibu wa sheria ya pensheni na viinua mgongo za mwaka 1966.
“Wengi kati ya wapiganaji hao walipewa ajira katika vyombo vya Ulinzi na Usalama hususani Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania, Jeshi la Polisi na Jeshi la Magereza. Aidha, wapo walioshindwa kuajiriwa kutokana na sababu mbalimbali,”alisema Dk. Tax.
Aidha, Dk. Tax amesema wizara yake inaendelea kufuatilia hali zao ili kuchukua hatua stahiki, huku akiwataka wazee ambao hawanufaiki na huduma hizo, kuwasilisha taarifa zao ili wasaidiwe.
Leave a comment