Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linawashikilia watu wawili kwa tuhuma za kujaribu, kukata baadhi ya vyuma vya ngazi ya nguzo kwenye daraja la Tanzanite lililopo maeneo ya Salender jijini hapa. Anaripoti Rhoda Kanuti …(endelea).
Watuhumiwa hao ambao majina yao yamehifadhiwa kwa sababu za kiuchunguzi, walikamatwa tarehe 2 Aprili, 2022 saa 10 alfajiri wakiwa wanajaribu kufungua vyuma vilivyopo kwenye nguzo inayojulikana kama P9 ambayo ipo kwenye daraja hilo.
Akizungumza na wanahabari leo Jumatatu tarehe 4 Aprili, 2022 Kamanda wa Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Jumanne Muliro amesema watuhumiwa hao wanahojiwa kwa kina na watafikishwa kwenye vyombo vya kisheria kwa hatua zaidi pale uchunguzi utakapokamilika.
Aidha, amesema Jeshi hilo limewakamata watu wengine kumi waliokutwa chini ya daraja hilo, wakidai kuwa wanaokota vyuma chakavu kwa ajili ya biashara ya vyuma.
“Watuhumiwa hao pia wanahojiwa kwa kina ili kubaini malengo yao chini ya daraja hilo, yalikuwa ni nini na kuona kama wana uhusiano na wale waliokuwa wanajaibu kuiharibu baadhi ya miundombinu ya nguzo,” amesema Muliro.
Muliro ametoa onyo na kwamba halitamvumilia mtu au kikundi chochote kinachojihusisha kwa namna yoyote ile kujaribu kuharibu miundombinu ambayo imejengwa kwa manufaa ya umma.
Leave a comment