ELIMU ya Mlipa kodi inayotolewa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imefumbua macho wawekezaji ambayo imewavutia wawekezaji kuja kuwekeza nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Balozi wa kodi nchini, Subira Mgalu amesema hayo leo Julai 11, 2022 alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari alipotembelea banda la TRA wakati wa maonyesho ya Kimataifa ya Kibiashara ya 46 yanayofanyika katika Viwanja vya J.K. Nyerere Maarufu kama Sabasaba jijini Dar Es Salaam. Amesema Sera za TRA imetajwa kuwa chachu ya ongezeko la wawekezaji nchini baada ya kuzielewa sera hizo.
“Kwa taarifa nilizopokea wananchi wamejitokeza lakini kipekee hata wawekezaji wemejitokeza kupata elimu ya mlipa kodi na baada ya maelezo hayo wawekezaji wamevutiwa kuwekeza nchini kwetu hili linakwenda sambamba na mpango wa Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan.” Amesema Subira
Aidha Mgalu amesema ameshuhudi kitengo cha maadili cha Mamlaka hiyo ambacho kitawathibiti watumishi wa TRA ambao sio waaminifu.
“Kipo kitengo cha maadili ambacho kinatoa fursa kwa mlipa kodi kama wanaona mwenendo wa maofisa wanaoshughulika na kukusanya kodi sio nzuri wanakila sababu ya kutoa taarifa na zikashughulikiwa kama alivyosema Waziri wa Fedha Dkt. Mwigulu Nchemba alipokuwa anawasilisha Bajeti ya Serikali alivyosema kuwa bado wapo wafanyakazi sio waaminifu wanaweza kutoa makadirio makubwa lakini wanaporuhusu mazungumzo yanashuka kwa hiyo natoa wito kwa walipa kodi kushirikiana na mamlaka hii,” amesema.
Amesema kwenye idara ya sera na utafiti ya mamlaka hiyo itakuwa ikifanya uchunguzi wa namna ya kuongeza walipa kodi.
Kuhusu elimu kwa mlipa kodi Mgalu ametoa wito kwa watanzania kudai risiti kwa kila manunuzi huku wafanyabiashara wakitoa risiti kwa kila wanapofanya mauzo.
Amesema kuwa kwa namna ambavyo watanzania wanaelimika katika kulipa kodi ameanza mwaka mpya wa fedha ambao serikali inatarijia kukusana shilingi Tirioni 41.48 ili ituletee maendeleo kwenye sekta mbalimbali.
Ameongeza kuwa Mamlaka hiyo inawajibu wa kukusanya kiasi cha shilingi Tirioni 23 na pesa hizo ndio zitakazojenga miradi mbalimbali ya kimkakati na elimu bure pamoja na utoaji wa huduma za afya na miundombinu mbalimbali nchini.
Kwa upande wake Ofisa muelimishaji wa TRA,Peter Kipapa amesema kuwa kitengo hiko kimetembelewa na wageni wengi waliokuwa wanataka kujua namna ya ulipaji kodi nchini tanzania na kwamba wanaonesha kuridhishwa na utendaji wa mamlaka hiyo.
Leave a comment