WAZAZI na walezi wametakiwa kuwalea watoto wao katika misingi ya dini ili kuepukana na kizazi chenye ukatili na unyanyasaji hapo baadaye. Anaripoti Danson Kaijage,Dodoma…(Endelea).
Wito huo umetolewa na mshiriki wa mashindano ya kusoma maandiko matakatifi katika kitabu cha Quran Tukufu,Mohammad Kimanja baada ya kuibuka kuwa mshindi wa kwanza kati ya washindani kumi waliongia fainali katika Mkoa wa Dodoma.
Akizungumza baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa kwanza na waamuzi wa shindano hilo ambao ni Mohammed Boki na Said Id Said amesema kuwa ili kuwa na jamii bora ni lazima kuwepo na kizazi cha wacha Mungu.
Kimanja amesema kuwa wazazi na walezi wanatakiwa kuwajengea watoto wao kwa kuwahamasisha na kuwafundisha kuona umuhimu wa kusoma maandiko nataktifu na kuyatendea kazi.
“Watoto wanatakiwa kufundishwa na kujengewa hofu ya kimungu katika kutenda haki badala ya kumwacha mtoto kutembea kwa njia ambazo hazifai kwa maisha yake ya duniani na mbinguni.
“Kwa sasa tunashuhudia vikundi vya vijana ambao wanajiita panyaroad, panya kalowa na makundi mengine mbalimbali lakini hayo yote yanatokana na wazazi na walezi kushindwa kukaa karibu na watoto wao na kutowapa misingi mizuri ya neno la Mungu.
Kwa upande wake Sheikh wa Mkoa wa Dodoma, Alhaji Mustapha Rajabu, amewahimiza waumini wa Dini ya Kiislamu kuendeleza mkakati wa kutoa mashindano ya kuisoma Quran kwa lengo ya kukaa na neno la Mungu moyoni.
Aidha amesema kuwa kuna kila sababu ya waumini wa dini ya Kiislamu kutenga muda wa kusoma maandiko matakatifu kwa utulivu ili yaweze kuwajenga na kuwakuza kiimani.
Leave a comment