BARAZA la madiwani katika halmashauri ya mji Tunduma wilayani Momba mkoani Songwe, wameazimia kutoa adhabu ya kuwafuta kazi watumishi saba huku kati yao wakikatwa asilimia 15 ya mishahara yao baada ya kubainika kuwa na makosa ya ubadhirifu wa fedha za miradi ya maendeleo kwenye idara zao. Anaripoti Ibrahim Yassin, Tunduma…(endelea).
Awali madiwani hao waliwatuhumu watumishi 20 wa idara mbalimbali wakiwemo wakuu wa Idara ya afya, manunuzi, elimu sekondari kuhusika na ubadhirifu huo lakini baada ya kuunda timu ya uchunguzi walibainika watumishi saba kuwa na hatia.
Hatua hiyo ililazimu kuitishwa kwa baraza la dharura na kujigeuza kuwa kamati iliyotoa maamuzi hayo leo Jumamosi.
Akitoa maamuzi hayo mbele ya kikao hicho cha baraza, Mwenyekiti wa halmashauri ya mji huo, Ayoub Mlimba aliwataja watumishi hao saba kati ya 20 waliokuwa wakituhumiwa ni Mkuu wa idara ya elimu sekondari, Patricia Mbigili ambaye pia imeamriwa kukatwa asilimia 15 ya mshahara wake kwa kipindi cha miaka 3.
Aliwataja wengine kuwa ni Ronald Msangi ambaye ni afisa kilimo daraja la Kwanza aliyeamriwa kushushwa cheo, Obed Mwakalinga mkuu kitengo cha Manunuzi na Ibrahim Lyimo afisa Manunuzi daraja la pili hao wamefutwa kazi huku Raphael Simkonda ambaye ni mtendaji kata daraja la tatu akipewa adhabu ya kukatwa asilimia 15 ya mshahara kwa miaka mitatu.
Alisema watumishi wa mikataba Ally Farayo msanifu majengo (Architect) na Japhet Chota mkadiriaji majengo (QS) wamesitishiwa mikataba yao na kufukuzwa kazi.
Aidha, afisa mtendaji kata ya Mpemba, Evance Kisanko imeamriwa kwamba achunguzwe kutokana na makosa mbalimbali ya kiutendaji kwenye kata yake baada ya kudaiwa kujifanya kamanda wa polisi na kupiga watu.
Mlimba ambaye pia ni diwani kata ya Mwakakati alisema wapo waliosema madiwani Tunduma hawana meno lakini wao walikuwa hawakurupuki.
Alisema badala yake waliunda timu kuchunguza tuhuma hizo na baada ya kukamilika kwa uchunguzi waliitisha baraza la dharura na kutoa maamuzi hayo.
“Kwa watumishi wanaodhani Tunduma ni shamba la bibi …wasahau hilo,tupo makini kuhakikisha fedha zinazotolewa na Rais Samia zinafanya kazi bila kuibiwa,” alisema.
Hata hivyo Mlimba alimuomba muwakilishi wa katibu tawala mkoa kuwahamisha watumishi waliotuhumiwa kwenda nje ya mkoa kwani wengi wao wamekaa muda mrefu wakifanya kazi Tunduma hali iliyopelekea wafanye kazi kwa mazoea.
Kwa upande wake Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo, Philimon Magesa alisema baada ya kubaini uwepo wa ubadhirifu kwenye baadhi ya miradi aliitisha kikao cha baraza la madiwani nà kuunda timu ya uchunguzi ambayo ilimpelekea ripoti na kuitisha kikao cha dharura na kutoa adhabu hiyo kwa kufuata kanuni na sharia zilizopo.
“Ninawasihi watumishi wengine kuwa waaminifu na fedha za umma.
“Hatutawaomea huruma katika utoaji wa adhabu kwa mtumishi atakayebainika kufanya ubadhirifu wa fedha ama wizi wa vifaa vya ujenzi kwenye miradi ya maendeleo, tunataka nidhamu ya matumizi ya fedha ifuatwe”alisema Magesa.
Alisema kuhusu ombi la kumchunguza afisa mtendaji kata Mpemba kwa tuhuma mbalimbali ikiwemo kujifanya mkuu wa polisi mkoa, alisema amelichukua na kuahidi kulifanyia kazi.
Diwani kata ya Majengo, Frank Mponzi alisema maamuzi hayo yamezingatia kanuni za utumishi wa umma, na kwamba mtumishi akifanya kosa lazima baraza lichukue hatua ili halmashauri isonge mbele.
Leave a comment