WATANZANIA wametakiwa kujenga utamaduni wa kufanya utalii wa ndani ili kuinua pato la Taifa ikiwa ni pamoja na kujivunia rasilimali muhimu za nchi zilizopo. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma( endelea).
Ushauri huo umetolewa leo tarehe 16 Machi 2023 na Kamishina Msaidizi Mwandamizi wa Jeshi la uhifadhi TANAPA, Ofisi ya kiunganishi Dodoma, Dk. Noelia Myonga alipozungumza na waandishi wa habari juu ya umuhimu wa uhifadhi.
Dk. Noelia amesema Tanzania imebarikiwa kuwa na vivutio vingi ambavyo ni muhimu kuvitembelea na bahati mbaya zaidi watanzania waliowengi bado hawana mwamko wa kutembelea vivutio hivyo.
Amesema kwa sasa Tanzania ina hifadhi 22 ambazo kila hifadhi inamvuto wake na maajabu yake ambayo yanawavutia watalii kwa kufika na kujifunza mambo kadhaa.
Amezitaja hifanyi hizo kuwa ni Arusha, Burigi -Chato, Gombe, Ibanda -Kyerwa, Katavi, Kigosi, Kilimanjaro, Kisiwa cha Rubondo, Kisiwa cha Saanane, Kitulo, Manyara, Mikumi, Mhale, Uduzungwa, Mkomazi, Mto Ugala, Nyerere, Ruaha, Rumanyika Karagwe, Saadani, Serengeti na Tarangire.
“Kila hifadhi imekuwa na mvuto wake tofauti kabisa, mfano hifadhi ya Manyara kuna simba ambao wanapanda miti na ndege wazuri na waajabu, hifadhi ya Tarangire kuna tembo wengi na mibuyu mikubwa ambayo inavutia zaidi, hifadhi ya Saadani kuna kasa wakubwa na wa kijani na vivutio vingi katika hifadhi mbalimbali” ameeleza Dk. Noelia.
Pia amesema kuna utalii wa kihistoria jambo ambalo linaonekana kusahaulika huku akikumbushia sehemu za Kondoa Irangi, Kongwa kwenye sehemu za wapigania uhuru.
Anatoa mfano wa eneo la Kongwa ambalo kuna kisa cha tembo aliyezama katika kisima cha maji na kusababisha Dodoma kupewa jina hilo.
Aidha, amesema kuwa TANAPA kwa sasa wameanzisha vikundi vya hamasa pamoja na kutoa elimu kwa wanafunzi ili kuona umuhimu wa kuwafundisha umuhimu wa uhifadhi na faida zake.
Leave a comment