Zaidi ya raia 2000 kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) wameingia nchini kuomba hifadhi ya ukimbizi kufuatia machafuko yanayoendelea katika mikoa ya mashariki mwa DRC. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa…(endelea).
Kwa mujibu wa idara ya wakimbizi ya wizara ya mambo ya ndani nchini Tanzania, wakimbizi hao wameanza kuingia nchini tarehe 5 Machi mwaka huu.
Idara hiyo imeongeza kwamba kwa wastani wanapokelewa kati ya watu 100 hadi 300 kila siku.
Mkurugenzi wa idara ya wakimbizi nchini, Sudi Mwakibasi amesema kinachofanyika kwa sasa, ni Tanzania kutekeleza hitaji la msingi la kuwapokea wanaohitaji hifadhi.
“Hadi sasa tumepokea waomba hifadhi 2,643,” alisema Mwakibasi
Aliongeza kwamba kati ya hao, takriban 630 tayari wamehojiwa ili kuthibitisha uhalali wao na kupewa hifadhi katika kambi ya Nyarugusu mkoani Kigoma magharibi mwa Tanzania.
Wizara hiyo imeongeza kwamba kundi hilo linahusisha wakimbizi wapya walioingia moja kwa moja kutoka DRC pamoja na waliokuwa wakiishi nchini bila vibali.
Waomba hifadhi hao wamedai kuwa kinachowaondoa Kongo ni ongezeko la mashambulizii ya waasi wa kundi la M23 wanaokabiliana na majeshi ya serikali.
Akizungumza na waomba hifadhi hao, Mkuu wa mkoa wa Kigoma, Thobias Andengenye ambao awali walipokelewa na kanisa katoliki amewataka kuwa watulivu wakati suala lao likishughulikiwa.
Aidha, ametoa onyo kwa waomba hifadhi hao akiwataka kutoa taarifa za kweli wanapohitajika kufanya hivyo huku akitoa wito kwa wenyeji kuwa watulivu wakati huu.
Mkoa wa Kigoma hadi sasa unahifadhi wakimbizi wapatao 200,000 kutoka Jamhuri ya kidemokrasia ya Kongo na Jamhuri ya Burundi.
Leave a comment