WIKI mbili baada ya mauaji ya mtoto mwenye ualbino, mkoani Tabora, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), kwa kusirikiana na Shirika la Tabora ‘Vision Community Organization’ (TAVICO), imemtaka Inspekta Jnerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro, kuwasaka waliohusika na mauaji hayo. Anaripoti Jemima Samwel na Nasra Bakari, DMC … (endelea).
Mauaji hayo yanadaiwa kutokea kati ya tarehe 3 na 4 Mei 2021, kitongoji cha Usadala, kijiji cha Utemini, Kata ya Ndono, wilaya ya Uyui, mkoani humo.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salam, jana Jumatatu, terehe 17 Mei 2021, Mkurugenzi Mtendaji wa LHRC, Anna Henga amesema, wamefuatilia na kugundua mtoto huyo mwenye jinsia ya kiume anakadiliwa kuwa na miaka mitamo hadi sita.
“Jina lake wala makazi yake hayakuweza kufahamika lakini mwili wake uliokotwa na wanakijiji ukiwa umetelekezwa kwenye majani eneo la shamba karibu na dimbwi la maji.”
“Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo, mwili huo ulikutwa ukiwa umekatwa mikono yote miwili, macho yote mawili yameng’olewa, sikio moja la mkono wa kushoto limekatwa na sehemu zote za siri zikiwa zimeondolewa”, amesema Anna.
Hata hivyo, amesema licha ya Jeshi la Polisi ngazi ya wilaya kuthibitisha mwili wa mtoto mwenye ualbino na kuwa hakuna ndugu aliyejitokeza, LHRC imeshtushwa na usiri wa tukio hilo na ni jambo la kusikitisha kuona taarifa za tukio hilo hazikuwekwa wazi ili ndugu au jamaa wa marehemu wapatikane.
“Jeshi la polisi na wanakijiji walithibitisha marehemu hakuwa mkazi wa kijiji husika wala vijiji vya jirani kutokana na ukweli kwamba tulielezwa kuwa afisa mtendaji wa kata alifanya ukaguzi kwenye vijiji nane vya kata yake mbapo haikupatikana familia yoyote iliyopotelewa na mtoto mwenye ualbino.”
“Ilithibitishwa aliuawa sehemu nyingine na sehemu ya mwili wake ukatelekezwa kwenye eneo la kijiji cha usadala, hii ni kwa sababu kwenye eneo la tukio hakukuwa na viashiria vyoyote vya purukushani kuhusu mauaji wala damu” amesema.
Hata hivyo, Focus Magwesele, Mkurugenzi Idara ya Uwezeshaji Tavico, ameitaka viongozi wa serikali akiwemo IGP Simon Sirro na Waziri wa Mambo ya Ndani, George Sinbachawene kulifuatilia suala hili kwa kinana wahusika wakamatwe na kuchukuliwa hatua.
Pia, kuhakikisba taarifa kuhusu tukio hilo zinawekwa wazi kwa umma ili wahusika wapate taarifa sahihi juu ya ndugu yao au mtoto wao alipozikwa.
“IGP Sirro ahakikishe anachukulia jambo hili kwa umuhimu wa hali ya juu kama anavyochukulia matukio mengine ya kiharifu, Waziri wamambo ya ndani afuatilie kwa kina na atoe kauli ya serikali bungeni, tunapata mashaka pengine matukio kama haya bado yapo na yanafumbiwa macho” amesema Magwesele.
Kwa upande wa Mwenyekiti wa Chama cha watu wenye Ualbino Tanzania, Godson Mollel, amesema huko nyuma matukio haya yalipungua tangia lakini tukio la mtoto huyo linatishia usalama wa albino.
“Mwaka 2017 hayakuwepo kabisa haya mauaji lakini sasa inatuonyesha kuwa mauaji yameanza tena, haijalishi ni albino au mtu wa kawaida, kibinadamu ni suala linalotisha hasa kwa familia iliyokutwa na hilo tatizo na Jamii kwa ujumla, na Jamii zinapaswa kutoa ushirikiano kwenye masuala kama haya na vyombo na usalama pia” amesema Mollel.
Mollel ameiomba serikali kufuatilia kwa kina kabla jambo hilo halijawa kubwa tena.
Mwili wa mtoto huyo unadaiwa kukaa zaidi ya siku mbili kutokana na kuharibika kwake hali iliyosababisha hata madaktari kushindwa kuuchukua kwa ajili ya uchunguzi.Ulizikwa na serikali baadaya ndugu kutojitokeza.
Leave a comment