WANANCHI wasiokuwa na muda wa kwenda katika Uwanja wa Uhuru, jijini Dar es Salaam kuuaga mwili wa aliyekuwa Rais wa Awamu ya Pili wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi, wametakiwa kujitokeza katika viunga vya barabara ambavyo mwili wake utapita kwa ajili ya kutoa heshima zao za mwisho. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 1 Machi 2024 na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, akielezea njia ambazo mwili wa Hayati Mwinyi aliyefariki jana Alhamisi, utapitishwa ukitokea nyumbani kwake Mikocheni kwenda Msikiti wa Baraza la Waislamu Tanzania (BAKWATA) hadi Uwanja wa Uhuru ambako utaagwa kitaifa.
Chalamila ametaja njia ambazo mwili huo utapita, ukianzia nyumbani kwake Mikocheni-Shoppers-Morocco-Kinondoni hadi BAKWATA, ambapo utaswaliwa. Baada ya kuswaliwa utapitishwa kuanzia BAKWATA-Magomeni, Kigogo-Ilala-VETA-Chuo cha DUCE hadi Uwanja wa Uhuru.
“Kwa maeneo yote haya niliyoyataja, ni muhimu kabisa watu wajitokeza kwa wingi ili kumpungia mkono na kuaga kwa Barabarani kwa wale ambao hawatapata nafasi ya kwenda moja kwa moja uwanja wa Uhuru, pamoja na haya tunaamini ya kwamba watu wote watajitokeza katika uwanja huu mkubwa wa Uhuru ili tuweze kutoa heshima za mwisho kwa mpendwa wetu,” amesema Chalamila.
Rais Mwinyi, amefariki dunia leo Ijumaa tarehe 29 Februari 2024 majira ya saa 11:30 jioni, katika Hospitali ya Kumbukumbu ya Emilio Mzena, Dar es Salaam, alipokuwa akipatiwa matibabu ya ugonjwa wa Saratani ya Mapafu.
Mwili wake unatarajiwa kuzikwa kesho Jumamosi, Unguja visiwani Zanzibar.
Leave a comment