MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imetupilia mbali pingamizi la upande wa utetezi kwenye kesi ya uhujumu uchumi inayomkabili aliyekuwa Makamu wa Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu (TFF), Michael Wambura. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Leo tarehe 14 Februari 2019 Kelvin Mhina, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama hiyo ametupilia mbali pingamizi hilo kutokana na mahakama hiyo kutokuwa na mamlaka ya kuamua chochote kwenye kesi hiyo.
Upande wa serikali uliwakilishwa na Ester Martin ambapo upande wa utetezi umewakilishwa na Emmanuel Muga.
Awali Majura Magafu aliomba mahakama kutupilia mbali kesi hiyo kwa sababu mashitaka yote 17 yaliyopo mahakamani, hakuna shitaka hata moja lilolofunguliwa chini ya sheria ya uhujumu uchumi.
Alisema, mashitaka ambayo mteja wake ameshitakiwa nayo, yamefunguliwa chini ya kesi za kawaida za jinai ambayo yanamruhusu mshtakiwa kuyajibu. Kesi hiyo itatajwa tarehe 28 Februari mwaka huu.
Wambura ambaye amerejeshwa mahabusu ameshtakiwa kwa uhujumu uchumi moja ya mashataka yake yakiwa ni utakatishaji fedha.
Imedaiwa kuwa, kati ya 15 Agosti na Oktoba 21 mwaka 2015, katika Ofisi za TFF mshtakiwa alijipatia Sh. 25,050,000 kutoka TFF huku akijua fedha hizo ni zao la kosa la kughushi.
Amedaiwa pia kati ya 16 Machi na 21 Oktoba 2015 Wambura alijipatia Sh. 75,947,924 kutoka TFF wakati akijua fedha hizo siyo halali.
Leave a comment