WAKILI Mashaka Ngole amechukua fomu ya kuomba ridhaa kupitia Chama cha Wananchi (CUF) ili kimpitishe kuwa mgombea ubunge wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA). Anaripoti Selemani Msuya… (endelea).
Bunge la Afrika Mashariki linashirikisha wabunge tisa kutoka kila nchi ambazo ni Tanzania, Rwanda, Burundi, Kenya, Uganda, Sudan Kusini na DRC Congo.
Ngole ambaye pia ni Mwanasheria Mkuu wa CUF, amechukua fomu hiyo jana tarehe 3 Agosti, 2022 katika Makao Makuu ya CUF, Buguruni wilayani Ilala jijini Dar es Salaam.
Wakili huyo alisema amekaa na kijitathmini ambapo amejiona anatosha katika nafasi hiyo, hivyo iwapo chama chake kitampitisha hatawaangusha wana CUF na Watanzania kwa ujumla.
“Kwa sasa tupo kwenye hatua ya kuchukua na kurejesha fomu, baada ya hapo tutapata nafasi ya kuomba kura ndipo tutanadi sera zetu naamini wapiga kura watatuelewa,” alisema.
Alisema ameamua kutumia haki yake ya kikatiba kuomba ridhaa ya chama chake kuwakilisha katika Bunge la EAC ambalo linashirikisha nchi saba wanachama.
Ngole alisema iwapo chama kitampa ridhaa ya kugombea atahakikisha anatekeleza majukumu hayo kwa weledi na uaminifu.
Naibu Mkurugenzi wa Mipango na Chaguzi CUF, Yusuph Mbungiro alisema hadi jana wanachama sita wa chama hicho walikuwa wamechukua fomu ya kuomba Ubunge wa EAC.
Alisema mchakato wa uchukuaji na urejeshaji fomu umeanza Julai 20 na kikomo chake kitakuwa Agosti 15.
Mbungiro alisema baada ya mchakato huo kukamilika hatua za ndani ya chama zitafuata ikiwemo kupitia fomu za wagombea na baadae Baraza Kuu la CUF litachagua watatu wa kwenda mbele.
“Hadi sasa tumetoa fomu sita kwa wanachama wetu wa CUF, nitoe rai kwa mwanachama yoyote anayetaka kugombea nafasi hiyo kujitokeza.
Sisi tunataka mwanachama hai, ambaye ni Mtanzania aje kuchukua fomu, kwani ni haki yake kikatiba,” alisema.
Naibu huyo alitoa rai kwa wanachama wanaochukua fomu kutofanya kampeni hadi michakato ya ndani ya chama ikapokamilika.
Alisema iwapo atabainika mwanachama kufanya kampeni kabla ya muda uliopangwa hatua za kisheria zitachuliwa.
Leave a comment