JAMII imetakiwa kujikita katika uzalishaji wa taulo za kike za kufua ‘Pedi’, ili kuimarisha hedhi salama kwa watoto wa kike, pamoja na kuhifadhi mazingira. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Ushauri huo umetolewa katika mafunzo ya utengenezaji pedi hizo, yaliyoandaliwa na Shirika la Urithi Wangu ( My Legacy), kwa ufadhili wa Shirika la Habitat for Humanity Tanzania na kufanyika jijini Dar es Salaam, kuanzia tarehe 27 Hadi 29, Aprili 2023.
Akizungumza katika mafunzo hayo yaliyotolewa kwa walimu 30 kutoka shule za msingi na sekondari kutoka wilayani Kinondoni, jijini Dar es Salaam, Mratibu wa My Legacy, Amina Mtengeti, amesema uzalishaji wa pedi hizo ukiongezeka utasaidia kupatikana kwa gharama nafuu.
Amesema, pedi hizo kwa sasa hutengenezwa na watu wachache ndiyo maana gharama zake ni kubwa na kwamba ili kupunguza gharama Shirika lake limeamua kusambaza ujuzi wa kuzitengeneza kwa watu ili uzalishaji wake uongezeke.
“Tumeanza kufundisha walimu wa shule za Kinondoni kutokana na ukata wa rasilimali fedha lakini tunaendelea kutafuta wafadhili ili tutor elimu hii kwa watu wengi zaidi. Lengo jamii ijue kuzitengeneza ili zizalishwe kwa wingi kitendo kitakachopelekea kuuzwa kwa gharama nafuu,” amesema Mtengeti.
Amesema walimu wanapewa mafunzo hayo, watakwenda kuwafundisha wanafunzi namna ya kuzitengeneza, jambo litakalowasaidia wanafunzi wa kike kuondokana na changamoto ya kukosa hedhi salama na kutohudhuria shule wakiwa katika kipindi hicho.
Mratibu huyo wa My Legacy, amesema kwa sasa watoto kike na wanawake wengi wanakabiliwa na changamoto ya kukosa hedhi salama, kutokana na kushindwa kumudu gharama za Kupata pedi za kawaida, hususan wanaoishi maeneo ya vijijini.
Amesema baadhi Yao hutumia majani kujistiri wanapokuwa katika hali hiyo kitendo kinachohatarisha usalama wa maisha yao.
Mbali na mafunzo ya utengenezaji pedi hizo, Mtengeti amesema walimu wamepewa mafunzo juu ya namna ya kutekeleza mradi wa usafi na mazingira ya ufundishaji (Wash), ikiwemo kuingizwa vipengele vyake katika masomo ya darasani.
Kwa upande wake Floragivalanah Clement, kutoka Shirika la Flowee, linalojishighulisha na utengenezaji wa pedi za kufua, amesema sodo hizo zinasaidia kupunguza gharama kwa kuwa zinadumu kwa muda wa miezi 12.
Clement amesema utengenezaji wake ni rahisi kwa kuwa vifaa vyake vinapatikana nchini, ikiwemo pamba na vitambaa vingine.
“Kuzitengeneza ni rahisi mtu anaweza Shona kwa sindano ya mkono, lakini pia vifaa vyake vya kutengenezea vinapatikana,” amesema Clement.
Leave a comment