WAFUGAJI hapa nchini wameshauriwa kuzingatia matumizi ya dawa za mifugo wanayopewa na wataalamu ili kuongeza kipato na kuboresha uchumi wao na Taifa kwa ujumla. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Wito huo ulitolewa na Mkurugenzi wa Kiwanda cha usambazaji Dawa za Mifugo na Kilimo nchini Farmbase Ltd, Suleiman Msellem wakati akimuelewesha Mkuu wa Wilaya ya Kilindi mkoani Tanga, Sauda Mtondoo alipotembelea banda hilo lililopo kwenye maonesho ya wakulima ya Mwalimu Nyerere 88 Kanda ya Mashariki.
Msellem amesema, kwa kufuata ushauri wa kitaalam na kutumia dawa ya kuogeshea mifugo inayotengenezwa na kampuni hiyo ijulikanayo kama Paranex inayodhibiti magonjwa ya mifugo kwa asilimia 80 kutasaidia wafugaji kumudu na kutotetereka na ufugaji.
Amesema, dawa hiyo inayopatikana Tanzania pekee kati ya nchi za Afrika Mashariki kwa mara ya kwanza awali ilikuwa ikipatikana nchini Uswis Pekee ambapo kufuatia Kiwanda hicho kuanza kuizalisha hapa nchini inapatikana kwa bei nafuu kwa ajili ya wafugaji wa hapa nchini na nchi za jirani.
Hivyo amesema kuwa dawa hiyo inayouzwa kwa bei ya sh 35,000 hapa nchini kunawezesha wafugaji kutoka nchi zingine kuinunua kutoka Tanzania na hivyo kuiingizia nchi mapato tofauti na zamani walikuwa wakinunua nje ya nchi na kupeleka fedha huko.
Pia amesema, dawa hiyo husaidia hata kwa kuzuia magonjwa kwa mazao shambani kama ikitumiwa wakati wa kuandaa shamba na kwamba Farmbase ilishawahi kwenda kutoa elimu kwa msimu wa kilimo wa mwaka jana katika mikoa ya Pwani na Morogoro pindi walipokumbwa na changamoto ya wadudu waharibifu wa mazao shambani.
Hata hivyo Msellem amesema, Farmbase inampango wa kuhakikisha dawa nyingi zaidi zinazalishwa katika Kampuni hiyo ambayo tayari imeshaanza kufanya kazi kwa kasi ili kusaidia wafugaji kupata dawa na utaalam kwa wepesi na pia kuboresha mapato ya nchi.
Awali Mkuu wa Wilaya ya Kilindi mkoani Tanga Sauda Mtondoo aliwashauri wasambazaji hao kuona umuhimu wa kufungua matawi yao maeneo mbalimbali hasa walipo wakulima na wafugaji ili kuweza kuwarahisishi upatikanaji wa huduma hizo muhimu.
Mtondoo amesema, kutomsogeze huduma mkulima au mfugaji kumesababisha watu kuzikosa na pengine kutumia wanazopata mbali kidogo na bila kuzingatia kiasi kamili wakizilinda zisiishe na hivyo kutoleta ufanisi unaokusudiwa.
Akizungumza katika Maonesho hayo mfugaji mmoja Richard Rwegerela ameiomba Serikali kuangalia namna ya kuiunga mkono Farmbase kufuatia kujikita katika kuzalisha dawa za mifugo na kilimo na kuweza kuwakomboa wakulima na Taifa kwa ujumla.
Leave a comment