WAFANYABIASHARA waliopoteza mali zao katika ajali ya moto iliyotokea kwenye Soko la Kariakoo, maeneo ya Mnadani, wameiomba Serikali iwasaidie ili waweze kupata mitaji. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Ombi hilo limewasilishwa leo tarehe 2 Oktoba 2023 na Mwenyekiti wa Wafanyabiashara wa Kariakoo, Martin Mbwana, kwa niaba yao wakati wanafanya zoezi la kuokoa mali zilizonusurika kuungua katika ajali iliyotokea asubuhi ya jana Jumapili.
Mbwana alidai kuwa, ajali hiyo imewaachia msiba wafanyabiashara zaidi ya 1,500 ambao vibanda vyao pamoja na mali vimetekekea kwa moto.
“Kuna wafanyabiashara zaidi ya 1,500 ambao ghafla bin vuu wamekosa biashara, wito wangu kwa Serikali kuja kukaa nao tuwape pole na kuona namna gani wanawasaidia. Huu ni msiba mkubwa moto umeharibu biashara zao zote,” amesema Mbwana.
Katika hatua nyingine, Mbwana ameiomba Serikali iunde timu kwa ajili ya kuchunguza chanzo cha moto ili kibainike kwa ajili ya kuchukua hatua za kudhibiti matukio ya moto kwenye soko hilo.
“Inabidi tuweze kujua moto huu chanzo chake na tukomeshe maana sasa imeshakuwa mazoea Kariakoo moto unatokea ndani ya mwaka mmoja mara tatu. Hii inaathiri mitaji ya watu sisi tunataka tushirikiane nao tukomeshe maana imeshakuwa mazoea,” amesema Mbwana.
Leave a comment