MAJALIWA Jackson, mvuvi aliyesaidia zoezi la kuwaokoa manusura wa ajali ya ndege ya Kampuni ya Precision Air mkoani Kagera, amechangiwa pesa kiasi cha Sh. 5,023,000 na baadhi ya wabunge kwa juhudi zake za kunusuru maisha ya watu 24.Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Wabunge hao wamemchanga fedha hizo leo Ijumaa, tarehe 11 Novemba 2022, baada ya Spika Dk. Tulia Ackson, kutoa muongozo uliowaomba wabunge wenye nia kumchangia Majaliwa ambaye alikuwepo Bungeni hapo, kufanya hivyo.
Akitangaza kiasi hicho cha fedha, Spika Tulia amemtaka Majaliwa, kuwakumbuka watu waliomsaidia kuokoa maisha yake, baada ya hali yake kuwa mbaya alipofanya zoezi hilo.
Spika Tulia alitoa muongozo huyo, baada ya Mbunge wa Nzega Vijijini, Dk. Hamisi Kigwangalla, kumuomba atoe muongozo wa kila mbunge kutoa Sh. 50,000 katika posho ya kikao cha leo, kwa ajili ya kumpa Majaliwa kama sehemu ya kutambua mchango wake kwenye kuokoa maisha ya wahanga wa ajali hiyo iliyotokea Jumapili ya tarehe 6 Novemba mwaka huu.
“Kwa kutumia kanuni zetu kama anakusudia kufanya hicho alichokifanya alipaswa atoe hoja wabunge muunge mkono halafu tuendelee, sababu hajafanya hivyo na kaniomba muongozo, muongozo wangu ni kwamba sababu kijana yuko bungeni, wahudumu watapita toeni michango apewe kijana wetu,” amesema Spika Tulia.
Majaliwa alisaidia zoezi la uokoaji katika ajali hiyo, baada ya kuufungua mlango wa ndege na kufanikisha kuokolewa kwa abiria 24 waliokuwa ndani ya ndege iliyotumbukia katika Ziwa Victoria, baada ya kushindwa kutua katika Uwanja wa Ndege wa Bukoba kutokana na hali ya hewa mbaya.
Leave a comment