BAADHI ya wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), wamesema hatua ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kukubali marekebisho ya sheria za uchaguzi imeonesha dhamira yake ya kutafuta maridhiano na kuijenga upya Tanzania. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Maoni hayo yalitolewa jana Ijumaa, baada ya muswada wa Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani wa 2023; Muswada wa Sheria ya Tume ya Uchaguzi wa 2023 na Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Vyama vya Siasa wa 2023, kupitishwa bungeni jijini Dodoma kwa ajili ya kuwa sheria baada ya kusainiwa na Rais Samia.
Mbunge viti maalum, Dk. Pauline Nahato alisema miswada hiyo imebeba maoni ya wadau juu ya maboresho ya mifumo ya uchaguzi, hasa kifungu kinachopendekeza mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi, kupendekezwa badala ya kuteuliwa moja kwa moja na Rais.
“Siku ya leo (jana) imekuwa ya kipekee sana katika Bunge letu kwa sababu imekuwa ni siku ambayo tumeijadili na kuridhia miswada iliyoletwa bungeni ambayo imepitia michakato muhimu sana.
“Napenda kumshukuru Rais Samia kwa kuridhia miswada kuja bungeni na kujadiliwa kwa uwazi kabisa. Kabla ya kuja bungeni imejadiliwa na watu wa makundi mbalimbali, wanasiasa, viongozi wa dini na wa vyama vyote,” amesema Dk. Nahato.
Naye Mbunge Viti Maalum mkoani Lindi, Maimuna Pathan, alisema miswada hiyo imebaba maoni yote yaliyotolewa na wadau na kwamba hakuna pendekezo lililoachwa.
“Mama yetu, Rais wetu Dk. Samia amefanya kitu ambacho anastahili sana apewe maua yake. Ni kitu kikubwa anatakiwa apongezwe ameonyesha mshikamano na ushirikiano, amekubali kupokea maoni yaliyotoka kwa wadau wote nje kwa wapinzani na waliomo ndani ya chama na watu mbalimbali. Amefanyia kazi bila kuyabagua ameyaleta bungeni yamejadiliwa kwa uwazi na kupitishwa,” amesema Maimuna.
Leave a comment