Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete amesema katika kipindi cha Julai 2022 hadi Desemba 2023, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) iliwachukulia hatua watumishi 51 kwa matumizi mabaya ya fedha za miradi 274 ya serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Kikwete ametoa kauli hiyo leo bungeni jijini Dodoma wakati akijibu swali la Mbunge wa Mbogwe, Nicodemas Maganga (CCM).
Maganga alihoji Je, Serikali inachukua hatua gani kwa watumishi wanaohusika na kutumia vibaya fedha za miradi ya Serikali?
Kikwete amesema Serikali imeendelea kuwachukulia hatua mbalimbali za kinidhamu watumishi wa umma wanaotumia vibaya fedha za miradi ya maendeleo ikiwemo kuwasimamisha kazi na kuwaanzishia mashauri ya kinidhamu.
“Mathalan, katika kipindi cha Julai 2022 hadi Desemba 2023, TAKUKURU ilifuatilia matumizi ya rasilimali za umma kwenye utekelezaji wa miradi 2,541 yenye thamani ya Sh 8.26 trilioni, ambapo miradi 467 ilibainika kuwa na mapungufu mbalimbali ikiwemo uvujaji na kutokuwa na thamani ya fedha,” amesema.
Amsema kutokana na matokeo hayo, hatua kadhaa zilichukuliwa kwa mujibu wa Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Sura 329, ikiwa ni pamoja na kuanzisha uchunguzi kwa miradi 274 ambapo Watumishi 51 walichukuliwa hatua za kinidhamu
“Ofisi yangu itaendelea kufuatilia utekelezaji wa Sheria na Kanuni ili kuhakikisha kuwa Watumishi wa Umma wanazingatia miiko na maadili ya utumishi wanapotekeleza miradi ya maendeleo na pamoja majukumu mengine katika Ofisi za Umma,” amesema.
Leave a comment