JESHI Polisi Mkoa wa Songwe liliwashikilia na kuwahoji viongozi wa watano wa Chama cha Ushirika wa Kilimo na Masoko (Amcos) cha Isaiso kilichopo Kata Ya Isaiso Wilaya ya Mbozi mkoani Songwe kwa ubadhilifu wa fedha za wakulima wa kahawa kiasi cha Sh. 160 milioni katika msimu wa kilimo 2022/2023. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Akizungumza jana tarehe 4 Juni 2023 Kamanda wa polisi mkoani Songwe, Theopista Mallya amesema viongozi hao wamekatwa kutokana na ufuatiliaji wa ubadhirifu wa fedha za wakulima wa kahawa katika vyama vya Ushirika wa Kilimo na Masoko (Amcos) vipatavyo 20.
Amewataja viongozi hao waliokamatwa tangu tarehe 23 Juni mwaka huu kuwa ni Mwenyekiti wa Bodi ya Amcos hiyo, Milton Mwampashi (53); Karani wa Amcos, Tilus Mwampashi (32) na wengine ni wajumbe wa bodi ambao ni Isack Mwamlima (50), Petro Halinga (51) na Emmanuel Kasekwa (51) wote ni wakazi wa Isaiso wilaya ya Mbozi Mkoa Wa Songwe.
Amesema ubadhirifu huo ulifanyika kwa njia mbalimbali Ikiwa pamoja na kuwalipa wakulima chini ya kiwango halisi katika kila kilo moja ya kahawa.
Amesema kupitia njia hiyo walifanya ubadhirifu wa kiasi cha Sh.49.9 milioni.
Aidha, Bodi hiyo inadaiwa kiasi cha Sh. 80 milioni ambazo waliwakopesha wakulima wasiojulikana na kisababisha Amcos ya Isaiso kupata hasara kutokana na upotevu wa fedha hizo.
Pamoja na hayo viongozi wa Amcos wakiongozwa na Mwenyekiti wa Bodi, Milton Mwampashi walijikopesha zaidi ya Sh 30 milioni pasipo kufuata utaratibu na kisha deni hilo kulihamishiwa kwenye Amcos.
Amesema Jeshi La Polisi Mkoani Songwe linaendelea kufuatilia ubadhilifu wa fedha za wakulima wa kahawa katika vyama vya ushirika wa kilimo na Masoko (Amcos) na hii ni utekelezaji wa timu pamoja na ukaguzi wa vyama hivyo Iliyoundwa na mkuu wa wilaya ya Mbozi, Ester Mahawe.
Leave a comment