Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega ameagiza kuondolewa katika nafasi yake Kaimu Mkurugenzi wa Uvuvi, Stephen Lukanga baada ya kushindwa kupanga na kutekeleza mikakati thabiti ya kukomesha uvuvi haramu nchini.
Ameagiza nafasi hiyo apewe aliyekuwa Mkurugenzi wa Idara ya Utafiti, Mafunzo na Ugani, Prof. Mohamed Sheikh. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Waziri Ulega ametoa uamuzi huo wakati akikabidhi boti 11 zenye thamani ya Sh 1. 85 bilioni zilizotolewa na Benki ya Maendeleo ya Kilimo (TADB) kwa mkopo kwa wavuvi wa Mkoa wa Dar es Salaam leo tarehe 28 Novemba 2023.
Ulega amefikia uamuzi huo baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa wadau wa uvuvi mkoani Dar es Salaam kuhusu kukithiri kwa vitendo vya uvuvi haramu katika ukanda Pwani hususani Dar es Salaam.
Tarehe 4 Oktoba 2023 akiwa mkoani Mwanza katika Soko la Lumumba, Ulega alimpa mwezi mmoja Kaimu Mkurugenzi huyo kuhakikisha anapanga na kutekeleza mikakati thabiti ya kukomesha uvuvi haramu nchini ambao kwa muda umekuwa ni kikwazo kwa maendeleo ya sekta ya uvuvi.
Leave a comment