Askofu Kanisa la Kiinjili, Kilutheri Tanzani (KKKT), Dayosisi ya Morogoro, Jacob Mameo ametoa wito kwa viongozi wenye tabia ya kutumia vibaya madaraka yao kuwakandamiza na kuwatesa watu wa tabaka la chini, kuacha tabia hiyo kwani sio tu chukizo kwa binadamu bali pia ni chukizo kwa Mungu Anaripoti Victor Makinda, Morogoro …(endelea).
Askofu Mameo ametoa wito huo wakati akizungumza kwenye ufunguzi wa kongamano la uzinduzi wa siku 16 za kupinga katili wa kijnisia lililoandaliwa na kanisa hilo.
“Vitabu vitakatifu vinaeleza kuwa tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, hivyo ni lazima maisha yetu yaenzi kusudi la uumbaji wa Mungu la kuishi kwa upendo, furaha kuwa sababu ya wengine kufurahia maisha,” amesema Mameo.
Aidha, ameongeza kuwa watawala wote nchini wanatakiwa wamuombe Mungu ili wasiwe chanzo cha kunyanyasa na kuumiza wengine kwa kuwa wana madaraka.
Amesema jamii ya Kitanzania na kote duniani iungane na kusema hapana dhidi ya vitendo vya ukatili wa kijinsia kwani vitendo hivyo huacha makovu makubwa yasiyofutika kwa wahanga.
Kongamano hilo lililowaleta pamoja viongozi wa dini, wanasheria, maafisa ustawi wa jamii wa Manispaa ya Morogoro na waandishi wa habari.
Aidha, Mratibu wa Mipango wa KKKT Dayosisi ya Morogoro, Yona Kitua amesema jamii inatakiwa iendelee kuelimishwa kwa lengo la kubainisha vitendo vipi vinaangukia katika ukatili wa kijinsia, madhara na nini kifanyike kuzuia vitendo vya ukatili wa kijinsia visiendelee kutokea.
“Ili jamii iwe salama pasipo vitendo vya ukatili wa kijinisia, lazima tuendelee kutoa elimu kwa mbinu mbali mbali na bila kuchoka, kwani elimu ndio njia pekee inayoweza kubadili tabia na mienendo isiyofaa kwenye jamii,” amesema Yona.
Afisa Utawi wa Manispaa ya Morogoro, Fidna Mathias amesema hakuna sababu ya jamii kufumbia macho vitendo vya ukatili wa kijinsia na kuwataka watu wote wanaofanyiwa vitendo hivyo au wanaoshudia mtu anafanyiwa vitendo hivyo kuripoti kwenye mamlaka husika.
Naye mmoja wa waandishi waliohudhuria kongamano hilo, Omary Hussen amesema dhima kubwa ya vyombo vya habari ni kusambaza elimu kwa jamii, hivyo wandishi wa habari wanapaswa kuhakikisha ujumbe unaotolewa kuhusu kupinga vitendo vya ukatali wa kijinsia unaifikia jamii yote.
Aliwaasa waandishi wa habari kote nchini, kuzitumia siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia kuandaa, makala na vipindi mbali mbali vya kuelimisha jamii kuendeleza mampambano ya kupinga vitendo vya ukatili wa kijinsia.
Leave a comment