WATUMISHI wa umma pamoja na wananchi katika wilaya ya Ukerewe mkoani Mwanza wameiomba serikali na mashirika yanayotoa huduma za jamii kusogeza huduma zake karibuili kupunguza gharama na muda kwenda mkoani, anaandika Moses Mseti
Wito huo umetolewa katika wiki ya maadhimisho ya huduma kwa wateja ya mfuko wa PSPF ambao umefungua ofisi zake wilayani Ukerewe.
Asilimia 80 ya wananchi wake wanategemea uvuvi kama njia kuu ya kuwaingizia kipato na kuongeza pato na wamekuwa wakifuata huduma ya PSPF jijini Mwanza.
Mmoja wa wananchi hao, ambaye ni mwalimu wilayani humo, Alestida Methew, amesema mara nyingi wamekuwa wakipata wakati mgumu kufuatilia fao la uzazi pindi wanapojifungua kwa kuvuka na meli kutoka visiwani kwenda jijini Mwanza.
“Tumekuwa tukipata usumbufu sana kufuatilia fao la uzazi na unakuta mtu umejifungua mtoto (kichanga) na bado haujapata nguvu za kutembea, lakini kwa sababu ya shida inakulazimu kufika Mwanza kufuatilia lakini kwa ufunguzi huu utatuondolea kero hizi,” amesema Methew.
Mkurugenzi mkuu PSPF, Gabriel Silayo amesema mfuko huo umesogeza huduma zake kwa wakazi wa kisiwa hicho ili kuwaondolea adha watumishi zilizokuwa zikiwakabili ikiwemo huduma za pensheni.
Amesema kwa muda mrefu wamekuwa wakipokea maoni kutoka kwa wanachama na wadau mbalimbali wakiwaomba PSPF kusogeza huduma zao karibu, hivyo kwa ufunguzi wa ofisi hizo ni utekelezaji wa maombi ya wanachama wao.
“Katika kuhakikisha kila Mtanzania ananufaika na PSPF tunatambulisha mpango wa uchangiaji wa hiari kwa wakazi wa Ukerewe, mpango huu ni fursa kwa Watanzania wote kujiunga na ni kwa watu wote waliopo sekta rasmi na wale ambao siyo rasmi,” amesema Silayo.
Leave a comment