WAFUGAJI katika wilaya ya Mvomero Mkoani hapa wametakiwa kufuata maelekezo wanayopewa na maofisa kilimo na mifugo juu ya ufugaji wa kisasa ili kupunguza migogoro ya ardhi, anaandika Christina Haule.
Ombi hilo lilitolewa juzi na mshiriki wa mdahalo wa elimu shirikishi kwa Umma juu ya utatuzi migogoro ya ardhi Ramadhani Saidi iliyohusisha washiriki kutoka kata za Hembeti, Mvomero na Dakawa ulioandaliwa na Chama Cha Wanahabari mkoani Morogoro (Moro Pc) katika mradi wa kuhamasisha amani uliofadhiliwa na The Foundation For Civil Society.
Saidi amesema kuwa licha ya kuwa maofisa kilimo na mifugo wa wilaya wamekuwa wakitoa elimu mara chache kwa wafugaji hao lakini walipaswa kuizingatia na kuitumia ili waweze kupunguza migogoro ya ardhi na pengine ya wakulima na wafugaji inayosababishwa kwa kiasi kikubwa na ongezeko la mifugo.
“Mfugaji ndio chanzo cha migogoro na sio mkulima sababu yeye ndio anamfuata mkulima kulishia mifugo ambayo amefuga ikiwa mingi na hivyo hawafuati sheria zilizopo na wakijikuta wameharibu wanatumia fedha zao kuzinunua sheria,” amesema Saidi.
Aidha aliwahimiza maofisa hao kujenga tabia ya kutoa elimu mara kwa mara kwa wafugaji na kuondoa ukakasi wa usimamizi wa sheria zilizopo.
Naye Anna Almasi ambaye ni mfugaji aliiomba Serikali kuweka mipango makini ya kudhibiti migogoro kwa kutenga maeneo ya wakulima na wafugaji na kusimamia kufuatia ugomvi unaotokea mara kwa mara kuwa unarudisha nyuma maendeeleo ya Familia.
Mwenyekiti wa (MoroPc) Nickson Mkilanya aliwaomba wafugaji na wakulima wilayani humo kujenga tabia ya kumaliza migogoro inayowakabili kwa amani.
Mkilanya amesema, suala la migogoro linapaswa kumalizwa kwa mawasiliano mazuri na sio kuwindana na pengine mapigano kwani yanasababisha uvunjifu wa amani.
Leave a comment