SERIKALI ya Ujerumani imeongeza muda wa mkataba wa ushirikiano wake na Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) katika masuala mbalimbali ya kuimarisha ulinzi na usalama nchini. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa jana tarehe 9 Mei 2019 kwa umma na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa, ikisema kwamba Serikali ya Ujerumani imeongeza muda wa miaka minne baada ya muda wa mkataba uliopo kutarajiwa kumalizika mwaka 2021.
Taarifa ya Msigwa inaeleza kuwa, Serikali ya Ujerumani kupitia Balozi wake wa hapa nchini, Dk. Detlef Waechter wakati akizungumza na Rais John Magufuli Ikulu jijini Dar es Salaam, imekubali kuongeza kipindi cha miaka 4 cha kutoa misaada kwa JWTZ kuanzia mwaka 2021 hadi 2024.
Kwa mujibu wa taarifa ya Msigwa, Dk. Waetcher ameahidi kwamba Serikali ya Ujerumani itaisaidia JWTZ kujenga Hospitali ya Kijeshi ya kiwango cha ngazi ya nne ‘Level 4’ mkoani Dodoma, itaongeza mafunzo kwa wanajeshi na vifaa vya ulinzi wa amani.
“Serikali ya Ujerumani itaendelea kufundisha madaktari wa Jeshi na kutoa vifaa vya matibabu na kutoa mafunzo ya ulinzi wa amani,” inaeleza sehemu ya taarifa ya Msigwa ikimnukuu Dk. Waechter.
Rais Magufuli ameishukuru Ujerumani kwa kuendeleza na kukuza uhusiano na ushirikiano na Tanzania na kumhakikishia Balozi Waechter kwamba serikali itahakikisha misaada yote inayotolewa inaleta manufaa yaliyokusudiwa.
Katika mkataba wa ushirikiano baina ya JWTZ na Ujerumani unaotarajia kuisha mwakani, kulijengwa Hospitali ya Kanda Monduli mkoani Arusha ambayo imewekewa vifaa tiba vya kisasa, upanuzi na uboreshaji wa Chuo cha Sayansi na Tiba cha Lugalo.
Vile vile, katika utekelezaji wa makataba huo ulifanyika ujenzi wa karakana za Jeshi katika mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma na Shinyanga, Ujenzi wa Idara ya Dharula ya Hospitali Kuu ya Jeshi Lugalo.
Leave a comment