BUNGE limeelezwa kuwa, polisi hatakiwi hatakiwi kumpiga au kumtesa mtuhumiwa wa makosa mbalimbali, wakati akiwa mikononi mwake au kwenye Kituo cha Polisi. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Hamadi Masauni, Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi ametoa kauli hiyo leo tarehe 10 Mei 2019 bungeni wakati wa maswali na majibu.
Amesema, msingi wa kauli hiyo ni kwa mujibu wa sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai sura ya 20 kifungu cha 11. Ni wakati akijubu swali la Mbunge wa Chonga, Mohamed Juma Khatibu (CUF).
Khatibu alihoji, ni katika mazingira gani askari polisi anapaswa au kulazimia kumtesa mtuhumiwa wa makosa mbalimbali wakati akiwa mikononi mwake au Kituo cha Polisi?
Akijibu swali hilo Masauni amesema, kwa mujibu wa sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai sura ya 20 kifungu cha 11 kinaelekeza namna ya ukamataji.
Amesema, kufungu hicho mahususi cha ukamataji, hakimruhusu askari kumpiga au kumtesa mtuhumiwa wa makosa mbalimbali wakati akiwa mikononi mwa polisi au kwenye Kituo cha Polisi.
“Kanuni za kudumu za utendaji wa Jeshi la Polisi (PGO) zinakataza na kuelekeza utendaji kazi wa askari polisi ambapo askari yeyote anapobainika kufanya vitendo vya kumpiga au kumtesa mtuhumiwa, huchukuliwa hatua za kinidhamu ikiwemo kufukuzwa kazi na kufikishwa mahakamani,” amesema Masauni.
Leave a comment