EMMANUEL Macron, Rais wa Ufaransa ameafiki uamuzi wa Donald Trump, Rais wa Marekani kijitoa katika mkataba wa mabadiliko ya tabia nchi wa Ufaransa, anaandika Catherine Kayombo.
Macron amesema hayo katika mkutano mjini Paris alipokutana na Trump kuzungumzia tofauti na mitazamo yao kuhusiana na mkataba huo.
“Kuhusu tabia nchi tunajua tofauti yetu, Trump ana ahadi za uchaguzi alizowapatia raia wake na mimi pia nilikuwa na ahadi, lakini vitu hivi havipaswi kuturudisha nyuma ni muhimu kusonga mbele,” alieleza Macron.
Alisisitiza umuhimu wa kuweka makubaliano hayo kando ili viongozi hao watatue masuala mengine muhimu ikiwemo kusitishwa kwa mapigano nchini Syria na Iraq na kuongeza ushirikiano wa kibiashara.
“Marekani inahusishwa zaidi na vita vinavyoendelea nchini Iraq, tumekubaliana kuendeleza juhudi zetu pamoja hususani katika mipango baada ya vita,” aliongeza Macron.
Akizungumza na rais wa Ufaransa, Trump alidokeza kuwa huenda Marekani itabadili msimamo wake hapo baadae, lakini kwa sasa itasimamia uamuzi huo. “Kama mabadiliko yatafanyika itakuwa ni kwa heshima ya makubaliano ya Paris na urafiki kati ya nchi zetu husani katika biashara.”
Trump alijiondoa katika mkataba wa mabadiliko ya tabia ya nchi mnamo Juni 2017 katika kutekeleza ahadi aliotoa wakati wa kampeni alipokuwa akigombea urais mwaka 2016. Alidai mkataba huo utahujumu uchumi wa Marekani na kudhoofisha uhuru wa kibiashara katika nchi hiyo.
Aidha uamuzi huo ulipingwa na baadhi ya viongozi wa mataifa 20 makubwa duniani (G20) huku wakiweka ahadi ya kuidhinisha makubaliano ya tabia ya nchi licha ya Marekani kujiondoa.
Leave a comment