TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), imewataka wapiga kura katika uchaguzi mdogo wa ubunge na udiwani, unaotarajiwa kufanyika kesho Jumamosi, kutofanya mikusanyiko katika vituo vya kupigia kura. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Agizo hilo limetolewa leo Ijumaa, tarehe 8 Oktoba 2021 na Mwenyekiti wa NEC, Jaji Semistocles Kaijage wakati akielezea maandalizi ya uchaguzi huo.
Mwenyekiti huyo wa NEC amesema, Maadili ya Uchaguzi ya 2020, yanaelekeza wapiga kura kuondoka vituoni baada ya kupiga kura.
“Kwa mujibu wa maelekezo yaliyopo kwenye maadili ya uchaguzi ya 2020, wapiga kura watatakiwa kuondoka vituoni baada ya kupiga kura, hivyo tume ina washauri wananchi kujiepusha na mikusanyiko katika maeneo ya vituo vya kupigia kura,” amesema Jaji Kaijage.
Pia Jaji Kaijage, amevitaka vyama vya siasa vinavyoshiriki chaguzi hizo, kufuata kanuni na taratibu za uchaguzi.
“Tume inavikumbusha vyama vya siasa na wagombea kuhakikisha wanazingatia sheria, kanuni na taratibu za uchaguzi, iwapo kutakuwa na malalamiko yotyote yatakayojitokeza wahusika watatakiwa kufuata taratibu katika mamlaka husika,” amesema Jaji Kaijage.
Uchaguzi huo mdogo unafanyika katika Jimbo la Konde, Visiwani Zanzibar, Jimbo la Ushetu mkoani Shinyanga. Na katika kata za Vumilia (Tabora), Neruma (Mara), Lyowa (Rukwa).
Jaji Kaijage amesema uchaguzi huo utahusisha vyama vya siasa vitano, wapiga kura 191,152 walioandikishwa katika daftari la wapiga kura na vituo vya kupigia kura 529.
Amesema, kampeni za chaguzi hizo zilizoanza tarehe 20 Septemba 2021, zitafungwa leo saa 12.00 jioni.
Leave a comment