MSANII wa vichekesho Idriss Sultan, amefikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi na wenzake wawili wakikabiliwa na kosa la kuchapisha maudhui mtandaoni bila kibali. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Washitakiwa wengine ni Daktari Ulimwengu na Isihaka Mwinyimvua.
Washtakiwa hao wamesomewa makosa yao mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi na Wakili wa Serikali, Batlida Mushi leo tarehe 20 Machi 2020.
Katika kesi hiyo namba 60 ya mwaka 2020, Wakili Mushi amedai kuwa Idriss na wenzake wametendeka kosa kati ya Machi 8, 2016 na Machi 12, 2020 katika maeneo tofauti jijini Dar es Salaam.
Inadaiwa katika maeneo hayo, walirusha maudhui kupitia chaneli ya YouTube huku wakiwa hawana kibali cha Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
Baada ya kusomewa mashitaka hayo, washitakiwa wote wamekana, wameachiwa kwa masharti ya dhamana ya kuwa na mdhamini mmoja kwa kila mshitakiwa ambao wamesaini bondi ya Sh. 8 milioni kila mmoja.
Kesi imeahirishwa hadi tarehe 21 Aprili 2020 ambapo itarudi kwa ajili ya kusikilizwa.
Leave a comment