TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) nchini Tanania, imesema imepekua nyumbani kwa aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Bandari Tanzania (TPA), Desdedit Kakoko na kukuta fedha kidogo zaidi ya Sh.8.5 milioni. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Ni baada ya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, kumsimamisha kazi Jumapili ya tarehe 28 Machi 2021, kutokana na ubadhirifu wa fedha zaidi ya Sh.3.9 bilioni na kuagiza Takukuru kufanya uchunguzi haraka wa tuhuma dhidi yake.
Rais Samia, alitoa maagizo hayo, mara baada ya kupokea ripoti mbili za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) nay a Takukuru zote za mwaka 2019/20, Ikulu ya Chamwoni, mkoani Dodoma.
“Kufuatia maelekezo ya Rais na Amiri Jeshi Mkuu, Takukuru ilichukua hatua za haraka za kumshikilia Kakoko kwa uchunguzi dhidi yake. Zipo taarifa kwamba Takukuru ilipokwenda kukagua ilikuta kiasi cha dola milioni 1.6.”
“Taarufa hizo hazina ukweli, Tulipopekua tulikuta kiasi kidogo sana cha fedha dola za Marekani 3,000 (sawa na Sh.7 milioni) na Sh.1.5 milioni,” amesema Brigedia Jenerali John Mbungo, Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru.
Bosi huyo wa Takukuru amewataka wananchi kupuuza taarifa hizo kwani hazina ukweli wowote na uchunguzi huo nyumbani kwa Kakoko, ulizingatia taratibu za kisheria.
“Uchunguzi huu ulikwisha kuanza tangu Machi 2020 na uko hatua za mwisho kabisa ili hatua ziweze kuchukuliwa dhidi ya waliohusika na ubadhirifu wa fedha za Serikali ndani ya Bandari ya Tanzania,” amesema Mbungo
Akitoa agizo la kusimamishwa kwa Kakoko, Rais Samia alisema “imani yangu ni kwamba, kama kuna ubadhirifu ndani ya shirika na kwa ripoti ile uliyonipa jioni, kuna uibadhirifu Sh. 3.9 Bil. karibu Sh. 4 Bil. Waziri Mkuu(Kassim Majaliwa) alivyofanya ukaguzi walisimamishwa wa chini, naomba nitoe agizo la kumsimamisha mkurugenzi mkuu wa bandari halafu uchunguzi uendelee.”
Leave a comment