STEVEN Mangele maarufu Steve Nyerere ametangaza kujizulu nafasi ya Msemaji wa Shirikisho la Muziki Tanzania (SMT). Anaripoti Rhoda Kanuti, Dar es Salaam … (endelea).
Steve ametangaza uamuzi huo leo Ijumaa tarehe 25 Machi 2022 ikiwa ni siku mbili zimepita tangu Baraza la Sanaa na Taifa (Basata) kumzuia kuendelea na majukumu ya usemaji.
Basata lilimzuia Steve kuendelea na majukumu yake hayo aliyoteuliwa na viongozi wa SMT mapema mwezi huu na kuibua mpasuko miongoni mwa wasanii wa shirikisho hilo.
Mpasuko huo ulimfanya Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mohamed Mchengerwa kuingilia kati na kuagiza katibu mkuu wa wizara hiyo kuitaka Basata kushughulikia mgogoro huo pamoja na kushauri inavyopaswa.
Tarehe 23 Machi 2022, Basata ilitangaza kumsimamisha Steve kuendelea na kazi hiyo hadi hapo baadaye.
Hata hivyo, leo Ijumaa akizungumza na waandishi wa habari akiwa na viongozi wa shirikisho hilo akiwemo rais wake, Ado Novemba, katika Ofisi za Basata jijini Dar es Salaam, Steve ametangaza kujizulu.
“Nimejiuzulu kwa sababu sioni kama hizi kelele zina tija kwa Taifa, yanini… yanini nimeachia Taifa letu lina mambo mengi ya msingi na makubwa ya kumsapoti Rais Samia,” amesema Steve ambaye ni msanii wa vichekesho na kuigiza sauti za viongozi hususan ya Mwalimu Julius Nyerere.
Hata hivyo, amesema “tunapambana na Mama na mtoto, Stiglers Gorge, madarasa na mambo mengine mengi, alafu tena tugombanie usemaji, cheo ambacho hata mshahara wake siuoni.”
Leave a comment