NI ‘majibizano’! Ndivyo uanavyoweza kutafsiri kile kinachoendelea kati ya Rais wa Zanzibar, Dk. Hussein Mwinyi na aliyekuwa Waziri wa Utalii na Mambo ya Kale Simai Mohamed Said ambaye amejibu mkuu huyo wa nchi saa chache baada ya ‘kurusha mawe gizani’. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa aliyoitoa kwa umma jioni ya leo Alhmisi, Simai ambaye tarehe 26 Januari mwaka huu alitangaza kujiuzulu, amejinasibu kuwa alisema ukweli wakati anatangaza kung’atuka.
Kauli hiyo ya Simai imekuja baada ya mapema leo Rais Dk. Mwinyi kusisitiza kuwa kiongozi anapaswa kusema ukweli wakati anajiuzulu.
Akiwaapisha mawaziri wapya aliowateua hivi karibuni, Rais Dk. Mwinyi amesema “Kujiuzulu si jambo geni. Mawaziri wanajiuzulu kwa sababu ni suala la uwajibikaji… hizi nafasi si za mtu kukaa maisha. Jambo la muhimu ni pale mtu anapoamua kujiuzulu, kusema ukweli wa sababu za uamuzi aliochukua,” amesema Rais Mwinyi.
Hata hivyo, katika taarifa hiyo ya Simai alianza kwa kudadavua kuwa kiutamaduni, si busara kuhoji, kujibu, kuongeza ama kupunguza kauli ya Rais akitoa kwenye vyombo vya habari, labda ingekuwa ndani ya vikao vya Chama Cha Mapinduzi ama Baraza la Mawaziri.
Japo ya kusisitiza asingependa kufanya hivyo, Simai amefafanya kuwa aliteuliwa kuwa Waziri kutumikia Wazanzibari katika sekta ya utalii, ambayo inabeba zaidi ya 75% ya uchumi wa Zanzibar. Hii ni uhai wa Zanzibar na eneo nyeti.
“Kwanza, Mheshimiwa Rais amesisitiza kuhusu kusema kweli wakati wa kujiuzulu, jambo ambalo nimelifanya. Kweli kwamba nilimpa barua kujiuzulu. Kweli kwamba imani yangu ni kuwa mazingira ya kazi kwa upande wangu hayakuwa yakinipa uwezo kusimamia sekta hii muhimu kwa uhai wa uchumi wa Wazanzibari kwa kiwango ambacho ningependa kuona nakifikia.
“Kweli kwamba kukaa pembeni kutampa Mheshimiwa Rais nafasi kuwa na mtu atakayeweza kumsaidia kadiri ya maono yake. Hizo ni kweli tatu kama ambavyo Mheshimiwa Rais amesisitiza,” amesema.
Hoja ya pili kuhusu kukimbilia kwenye vyombo vya habari ambayo Rais Mwinyi ameonya, Simai naye amedai kuwa kiongozi ukishaandika barua kwa Rais kujiuzulu, ni vyema pia kuujulisha umma.
“Waziri ni mtumishi wa umma. Hivyo basi Mheshimiwa Rais yuko sahihi na ndicho nilichofanya. Kuandika barua na kisha kuujulisha umma,” amesema Simai.
Duh!
Sijui Afrika itaacha lini tabia za kikoloni za kunyamazisha watu kuongea. Mtu anapokua chini ya uongozi hawezi kukosoa. Lakini akishajiuzulu aachwe akosoe kwani hayupo chini ya uongozi. Afrika inauwa vipaji vingi sana kwa kunyamazisha watu.
Hii pia inaondoa uwezo wa watu kuwajibisha serikali…na kujenga utamaduni ule ule tulioupiga vita tupate uhuru. Sasa uhuru huo uko wapi?