WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema agizo la kufungwa kwa shule na vyuo vya kati na vya elimu ya juu, liliotolewa tarehe 17 na 18 Machi mwaka huu, litaendelea hadi pale serikali itakapotoa taarifa nyingine. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Waziri Mkuu amesema wamefikia maamuzi hayo kutokana na kuongezeka kwa idadi ya wagonjwa wa Homa Kali ya Mapafu, inayosababishwa na Virusi vya Corona (COVID-19), kutoka 49 hadi kufikia 53.
Kufuatia ongezeko hilo, Waziri Majaliwa amesema pia, Rais John Magufuli amesitisha maadhimisho ya miaka 56 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar, pamoja na Siku Kuu ya Wafanyakazi (Mei Mosi).
Taarifa hizo zimetolewa leo tarehe 14 Aprili 2020 jijini Dodoma, na Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu, wakati akizungumza na wajumbe wa Kamati ya Kitaifa ya Kuratibu mapambano dhidi ya COVID-19.
Waziri Majaliwa amesema, Rais Magufuli ameagiza kiasi cha Sh. 500 milioni zilizopangwa kufanyia sherehe za maadhimisho ya muungano, zipelekwe katika Mfuko wa Kupambana na ugonjwa huo, wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar.
Amesema sherehe hizo zimesitishwa ili kuzuia mikusanyiko, inayoweza sababisha kuenea kwa ugonjwa huo.
Leave a comment