KATIBU Mkuu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislam nchini Tanzania Sheikh Ponda Issa Ponda amesema vyombo vya habari vikiwa huru vinaisaidia Serikali kupata taarifa muhimu zitakazowezesha upatikanaji wa maendeleo. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza na MwanaHALISI Online leo tarehe 25 Oktoba, 2022 Sheikh Ponda amesema kuna umuhimu wa vyombo kuwa huru ili kuchagiza uhuru wa mawazo yatayotoa matokeo chanya kwenye taifa.
“Vyombo vya habari ni muhimu kwa serikali kwa sababu vinawawezesha kupata taarifa” amesema Sheikh Ponda.
Ametoa mfano wa Kamati iliyoundwa na Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini IGP Camillius Wambura ya kuchunguza mauaji ya Ikwambi mkoani Morogoro kuwa alipata taarifa kupitia vyombo vya habari vya kijamii.
IGP wambura ameunda kamati hiyo tarehe 24 Oktoba 2022. Siku moja tu baada ya taarifa za tukio hilo kutokea ambapo watu wawili wameripotiwa kuuawa na wengine wawili kujeruhiwa wakati askari wa jeshi hilo walipokuwa wakidaiwa kutuliza ghasia.
Licha ya taarifa hiyo Sheikh Ponda amesema Serikali inapata taarifa muhimu kutoka kwa waandishi wa habari.
“Serikali inapata taarifa nyingi na muhimu kutoka kwenye vyombo vya habari kwa sababu waandishi wanafika sehemu ambazo serikali haifiki”.
Amesema nchi yetu imekuwa nyuma ya muda kutokana na vyombo vya habari kutokwa huru “Jamii yetu ilikuwa nyuma kwa sababu taarifa zilikuwa zinatoka upande mmoja tu wa wanasiasa nafuu ilipatikana pale paliporuhusiwa vyombo vingi”.
Sheikh Ponda ametoa mfano kwenye uombaji wa leseni ya Utangazaji masafa ya utangazaji wa Radio kwamba mtu anapewa kikomo cha masafa ilhali angeruhusiwa kurusha nchi nzima isingekuwa tatizo.
“Magazeti yanafungiwa bila kuwa na sababu muhimu mtu anafungiwa kisa kuna habari haijawaridhisha wanasiasa ikiwa vyombo vyenyewe vichache,’ amesema.
Amesema kuwa anashangazwa na mamlaka kufungia vyombo vya habari muhimu kwa sababu za kisiasa.
Akizungumza umuhimu wa uhuru kwa ujumla Sheikh Ponda amesema kuyabinya mawazo ya watu wengine na kutaka maoni ya upande mmoja kumetoa maana ya nchi kuwa huru.
“Uhuru ni jambo muhimu watu walipoteza roho mali zao kupigania uhuru wetu, uhuru ni maendeleo unamponyima mtu uhuru unasababisha matatizo,” amesema.
“Sisi kwetu tunatatizo kwenye uhuru licha ya kupigania uhuru huo kutoka kwa wakoloni ” amesema Sheikh Ponda.
Leave a comment