KATIBU wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Shaka Hamdu Shaka, amesema ndani ya chama hicho hakuna mpasuko, kama inavyovumishwa na baadhi ya watu. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Shaka ametoa kauli hiyo jana Jumanne, jijini Dar es Salaam, alipotembelea ofisi za magazeti ya MwanaHALISI na Raia Mwema.
“Ndani ya CCM ni shwari, mambo yanakwenda vizuri na taratibu zote na kanuni za CCM zimekuwa zikitekelezwa kama ilivyo ada na hakuna tishio lolote ndani ya CCM labda kinachozungumzwa ni kuleta hofu kwa njia moja au nyingine na ikawa sehemu ya propaganda sababu CCM ni chama kikubwa huwezi kuongoza na wengine wakashindwa kuzungumza mambo,” amesema Shaka.
Katibu mwenezi huyo wa CCM, amesema CCM kinaendelea na majukumu yake ya kichama pamoja na ya kuisimamia Serikali iliyoko madarakani.
Alipoulizwa kuhusu mabadiliko ya katiba ya CCM yaliyofanywa hivi karibuni kama yameondoa kofia mbili za uongozi, Shaka amesema “ni kweli tumefanya mabadiliko ya katiba ya CCM, nadhani kanuni bado haijabadilika na ukisoma kanuni ya 23 za uchaguzi wa CCM inasema nafasi moja ya uwakilihsi ni kofia moja tu.”
Katika hatua nyingine, alipoulizwa kama CCM kitaendelea kuteua watu wanaotoka upinzani badala ya wanachama wake waliopambana katika uchaguzi, Shaka amesema utaratibu huo utaendelea kutumika kwani chama hicho ni mlezi na kimbilio la watu.
“Sisi tunaongozwa na ahadi ya mwanachama, ukisoma katiba ya chama kwenye ahadi za wanachama ambazo ukisoma ukizifahamu vizuri huna sababu ya kujipa hofu. Kanuni inasema kwamba sisi wote ni ndugu na Afrika ni moja. Hii peke yake imetosha kwa sababu chama hiki ni kimbilio watakwenda huko mwisho wa siku watarudi CCM,” amesema Shaka.
Shaka amesema “na wanaokwenda huko watarudi wanakwenda kuchungulia mwisho wa siku wanarudi nyumbani. Kwa dhati tunakwenda vizuri na wakija naweza kuwahakikishia tunakwenda vizuri mno na hamna haja ya kuwa na hofu.”
Akizungumzia kuhusu uchaguzi wa ndani wa CCM, Shaka amesema unakwenda vizuri na kwamba mwitikio wa walijitokeza kuwania nafasi mbalimbali umekuwa mkubwa hasa kwa wanawake na vijana.
“Kwenye suala la uchaguzi tunakwenda vizuri, kuanzia tarehe 2 Julai 2022 tumeanza kutoa fomu ngazi ya wilaya, mkoa na taifa. Mwitikio ni mkubwa mno kwa mara ya kwanza wanawake mwitikio wao wa kujitokeza kuomba nafasi ya kuaminiwa ndani ya chama umekuwa mkubwa na wa vijana, Ijumaa tutakuwa tumepata namna kwa uhakika wangapi wamejitokeza,” amesema Shaka.
Leave a comment