Naibu Waziri wa Nishati, Judith Kapinga amewaomba Watanzania waendelee kuvumilia makali ya mgawo umeme hadi tarehe 16 Februari mwaka huu ambapo majaribio ya uzalishaji wa umeme kutoka katika Bwawa la Mwalimu Nyerere yatakuwa yamnekamilika. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Amesema baada ya majaribio hayo, wanategemea kuanza kupata megawati 215 za mwanzo hivyo umebaki muda mchache ukilinganisha na hali ilivyokuwa huko nyuma.
“Tuvumilie ili tuweze kukamilisha zoezi hili ili kupata umeme wa uhakika,” amesema.
Kapinga ametoa kauli hiyo leo Alhamisi bungeni jijini Dodoma wakati akijibu maswali ya wabunge waliolalamika mgawo wa umeme katika majimbo yao licha ya mvua kunyesha na kusababisha mafuriko katika maeneo mbalimbali ya nchi.
Katika swali la msingi, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Aida Khenani (Chadema) alihoji je, Serikali ina mkakati gani wa kumaliza changamoto ya kukatika kwa umeme Wilaya ya Nkasi.
Akijibu swali hilo Kapinga amesema wilaya ya Nkasi inapata umeme kupitia njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 66.
Amesema kwa kutambua changamoto ya kutokujitosheleza kwa umeme, Serikali imeshaanza mradi wa kupeleka umeme kutoka Gridi ya Taifa kwa Mkoa wa Rukwa ambapo mkoa utapata umeme kupitia utekelezaji wa Mradi wa TAZA ulioanza kutekelezwa Novemba, 2023 na unatarajiwa kukamilika Agosti, 2026.
Hata hivyo, katika swali la nyongeza Khenani alihoji nini sababu nyingine ya umeme kukatikatika katika maeneo mbalimbali ya nchi licha ya serikali kudai changamoto ya kukatika kwa umeme inatokana na upungufu wa maji ambayo sasa maji ni mengi na mafuriko yametokea.
Naye Mbunge wa Mbagala, Abdallah Chaurembo (CCM) alihoji Serikali iweke wazi ni nini sababu za msingi za kukatika kwa umeme katika eneo hilo.
Pia Mbunge wa Kilombero, Abubakar Asenga (CCM) alidai licha ya eneo lake kuwa na migopi ya Kidatu na Kihansi ya kuzalisha umeme cha ajabu kuna tatizo la mgawo wa umeme.
Aidha, Mbunge wa viti maalumu CCM, Stella Fiyao naye alidai kila mara umeme unakatika Songwe licha ya kuwa mkoa jirani na nchi za ukanda wa kusini mwa Afrika ambako biashara imepamba moto.
Akijibu maswali hayo, Kapinga alisema maeneo ya mabwawa ya kuzalisha umeme hayakupata mvua za el nino hapo awali, ambapo kiwacho cha uzalishali kipungua kutoka Megawati 426 hadi 254 lakini sasa kwa mvua zinazoendelea uzalishaji umeongezeka hadi Megawati 400.
Amesema kiujumla kuna upungufu 144 lakini Serikali inaendelea kuboresha hali ya upatikanaji wa umeme nchini.
Kuhusu Mbagala naibu waziri huyo amesema kwa kuwa ni eneo linalokua kwa kasi wameagiza mashine ili kutanua kituo cha kupoza umeme pamoja na kuimarisha miundindombinu, vivyo hivyo kwa upande wa Kilombero amesema Serikali inatarajia kujenga kituo cha kupoza umeme.
Leave a comment